MMOJA wa “vijana wa kazi” wanaotuhumiwa kushirikiana na aliyekuwa Kaimu Mkuu wa Polisi Mkoa wa Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Abdallah Zombe, katika mauaji ya watu wanne, ametiwa mbaroni baada ya kujisalimisha.
Mtuhumiwa huyo, Koplo Festus Bwabisabi, sasa anaunganishwa na wenzake 11 kujibu mashitaka hayo ya mauaji ya wachimbaji madini watatu wa Mahenge mkoani Morogoro, na dereva teksi mkazi wa Dar es Salaam.
Baada ya kujisalimisha Kisutu, haraka haraka, polisi walimuunganisha katika kesi hiyo, na kumsomea mashitaka kama waliyosomewa wenzake.
Mbele ya Hakimu Mwandamizi Mfawidhi, Sivangilwa Mwangesi, Mwanasheria wa Serikali, William Magoma, alimsomea mtuhumiwa mashitaka manne yanayomkabili.
Magoma alidai kuwa, Koplo Bwabisabi anatuhumiwa kwa mauaji ya wafanyabiashara watatu wa wilayani Mahenge na dereva teksi wa kituo cha Sinza, Dar es Salaam; uhalifu ambao alidai kwamba watuhumiwa waliufanya Januari 14, 2005 maeneo ya Msitu wa Mbezi Louis, Dar es Salaam.
Magoma aliwataja waliouawa kuwa ni Ephaim Sabinus Chigambi, Sabinus Chigambi (Jongo), Mathias Lunkombe; na dereva wa teksi, Juma Ndugu.
Pamoja na Zombe ambaye ndiye mshitakiwa namba moja, wengine ni Christopher Bageni, Ahmed Makele, Noel Leonard, Jane Andrew na Koplo Nyangelela Morris.
Wengine ni Koplo Emmanuel Mabula; E.6712 Felix Sandys Cedrick; Koplo Michale; D.2300 Abeneth, PC Michael; Rashid Mahmoud Lema; na D/CPL Rajabu Hamis Bakari.
Watuhumiwa wote wapo katika mahabusu ya Ukonga. Kesho kesi yao itanguruma Kisutu.
Julai 13, mwaka huu, watuhumiwa 11, akiwamo Zombe walifikishwa Kisutu. Ilielezwa kwamba kesho watafikishwa mahakamani kwa ajili ya kusomewa maelezo ya mashahidi, tayari kwa kusikilizwa na Mahakama Kuu.
Mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi Mfawidhi, Sivangilwa Mwangesi, Mwendesha Mashitaka, Charles Kenyela, aliiambia mahakama kuwa upelelezi wa kesi hiyo umekamilika.
Alisema baadhi ya watuhumiwa walioomba kuandika maelezo ya nyongeza, wamekamilisha na maelezo hayo yameshawasilishwa kwa Mkurugenzi wa Mashitaka nchini (DPP), tayari kwa kusikilizwa katika Mahakama Kuu.
Waliokuwa wameomba kuandika maelezo ya ziada ni Ahmed Makele, Jane Andrew, Christopher Bageni, PC Konstebo Michael, D 2300 Abeneth na Noel Leornad.