WALIODAIWA kuwa wafuasi wa Chama cha Wananchi (CUF), ambao walishitakiwa kwa kosa la kuchoma nyumba moto na kuua watu watano, eneo la Manzese Midizini, Kinondoni, wameachiwa huru na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.
Mbele ya Hakimu Mkazi, Sivangilwa Mwangesi, Mwendesha Mashitaka Inspekta Msaidizi, Boniface Edwin, alisema kesi hiyo imefutwa kwa amri ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP).
Hakimu Mwangesi alisema washitakiwa wameachiwa huru chini ya kifungu cha sheria 91, ibara ya kwanza katika kifungu kinachoelezea makosa ya jinai, ambacho kinaruhusu washitakiwa kuachiwa huru kwa amri ya DPP.
Mwendesha Mashitaka, Edwin aliwataja watuhumiwa walioachiwa huru kuwa ni pamoja na mganga wa kienyeji Rashid Mohamed, (44), Juma Rajabu (25), Hassan Kassim (37), Kasim Salum (55) na Juma Omari (32), ambao wote ni wakazi wa Manzese Midizini, Dar es Salaam.
Awali ilidaiwa kuwa Agosti 9, mwaka jana saa 8 usiku, eneo la Manzese Midizini, washitakiwa wote kwa pamoja walikula njama na walichoma moto nyumba ya aliyekuwa Katibu Mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), tawi la Midizini na familia yake na kusababisha kifo cha watu watano.
Waliokufa katika tukio hilo walikuwa ni Mwajuma Nyanza ambaye ni Katibu Mwenezi wa CCM Tawi la Manzese Midizini, Mwajuma Rashidi, Baibai Lucian, David John na Asha Rashid.
Kosa hilo lilihusishwa na mambo ya siasa, kwani lilitokea wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu na viongozi wengi wa CCM, akiwamo Rais Jakaya Kikwete, wakati huo akiwa mgombea urais wa CCM, alitembelea eneo hilo na kuahidi waliohusika wangechukuliwa hatua kali za kisheria.
Wafuasi wa CUF walihusishwa moja kwa moja na tukio hilo lililokuwa na mtazamo wa kisiasa.