KANISA Katoliki nchini hapa limetoa wito wa kususiwa kwa uchaguzi mkuu utakaofanyika Jumapili iwapo suala la hujuma halitashughulikiwa.
Kwa mujibu ya barua iliyosomwa na makanisa jijini hapa juzi, kuwapo kwa mkanganyiko juu ya idadi ya wapiga kura waliosajiliwa kunaweza kutumika kuuvuruga uchaguzi huo.
Ijumaa iliyopita, maaskofu wa Kikatoliki walisema kuwa hawatatambua matokeo ya uchaguzi huo isipokuwa tu pale ambapo kasoro zilizopo zitakapotatuliwa.
Zaidi ya nusu ya wakazi wa nchi hii iliyoathirika kwa vita ya wenyewe kwa wenyewe ni Wakatoliki.
Mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa, William Swing, alisema kuwa maandalizi ya uchaguzi huo yanaendelea vyema, japokuwa alisema kuwa kuna mengi zaidi yanayohitaji kufanywa.
Swing aliliambia Shirika la Habari la Uingereza, BBC kwamba UN iko makini lakini haina wasiwasi na hali ya usalama huku akitiwa moyo na ukweli kwamba hadi sasa wapiganaji waasi mashariki mwa nchi hawajaingilia kuvuruga mchakato wa uchaguzi huo.
DR Congo inaendesha uchaguzi mkuu wa kwanza wa kidemokrasia baada ya kudhoofu kwa vita ya wenyewe kwa wenyewe iliyomalizika mwaka 2003.
Hata hivyo watu zaidi ya 1,000 hufa kila siku, moja kwa moja au kutokana na machafuko hayo.
Viongozi wa Kikatoliki ni moja ya makundi yenye nguvu na ushawishi mkubwa nchini hapa yaliyotoa mwito wa kususiwa kwa uchaguzi.
Maaskofu hao wanadai kwamba Rais anayewania nafasi hiyo, Joesph Kabila, ametumia vibaya mali za serikali katika kampeni za uchaguzi kwa faida yake na anatumia vitisho kama silaha ya kisiasa.
Jingine linalotia hofu nchini hapa ni kwamba wagombea wengine wote wanaoongoza katika kinyang’anyiro cha urais walikuwa wababe wa vita walioisababishia nchi hii matatizo makubwa.
BBC