MWENYEKITI wa Halmashauri ya Wilaya ya Arumeru, John Saitabau, anatuhumiwa kuwakingia kifua ndugu zake wanaodaiwa kumjeruhi ndugu yao, Elias Saitabau, katika Kijiji cha Olgilai wilayani hapa.
Mwenyekiti huyo anadaiwa kuzuia mkono wa dola kuwakamata watuhumiwa hao licha ya tukio hilo kuripotiwa katika Kituo Kidogo cha Polisi Usa River na kufunguliwa jalada namba USR/IR/2378/06 Julai 12, mwaka huu.
“Angalia nilivyoumia kichwani, nimeshonwa nyuzi nane, kidoleni nyuzi mbili na tayari mgongo umetenguka hali inayonifanya nishindwe kuamka… yote haya yametokea baada ya mimi kuzuia miti yangu isikatwe,” alisema Elias ambaye yuko mafichoni akihofu kudhuriwa.
Aliongeza: “Nilipigwa mbele ya askari polisi watatu wa kituo kidogo cha Mbangata”.
Alidai kwamba waliompiga wote ni wanandugu, yaani Gabriel, Emmanuel na Hooshumu.
Akizungumza kwa njia ya simu na Tanzania Daima mwishoni mwa wiki, mwenyekiti huyo alikanusha tuhuma hizo.
“Siwakingii kifua kwa nia yoyote ile, na wala sihusiki kuwakamata na kuwafikisha mahakamani, suala hilo lipo polisi, naomba nisihusishwe kwa lolote,” alisema.