CHAMA cha Wananchi (CUF), kimekubali kuisamehe Serikali ya Marekani kwa kitendo cha kumshikilia mbunge wake wa Konde, Dk. Ali Tarab Ali katika Uwanja wa Ndege wa John F. Kennedy baada ya kumfananisha na gaidi anayesakwa na nchi hiyo.
Kaimu Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Mahusiano na Umma wa CUF, Mbaralah Maharagande, aliiambia Tanzania Daima jana kwa njia ya simu kuwa chama chake kimeipokea samahani iliyoombwa na Marekani.
Alisema wanasubiri kauli rasmi ya Mwenyekiti wa Taifa wa chama hicho, Profesa Ibrahim Lipumba ambayo itatolewa atakaporejea Dar es Salaam. Kwa sasa Profesa Lipumba yupo ziarani wilayani Lushoto.
“Tunasubiri tamko rasmi la mwenyekiti ambalo litatolewa kwa Watanzania wote atakaporejea kutoka Lushoto, tunatarajia kuandaa kikao maalumu cha chama ambacho kitatoa maamuzi ambayo yatakuwa rasmi,” alisema Maharagande.
Alisema kikao hicho pia kitapanga mikakati ya kuwalinda wabunge wake ili kuhakikisha kitendo hicho hakijirudii tena kwa viongozi wa chama hicho.
Maharagande alisema kitendo alichofanyiwa mbunge wake na maofisa usalama wa Marekani, hakikumuathiri yeye binafsi, bali kilikuwa na athari kubwa hata kwa chama chenyewe kwa kuharibu taswira yake.
Hivi karibuni, Balozi wa Marekani nchini, Michael Retzer alimwandikia barua ya kumuomba radhi, Spika wa Bunge, Samuel Sitta kutokana na kitendo kilichofanywa na maofisa usalama wa serikali ya nchi yake.
Katika barua hiyo, Retzer anaeleza kuwa, tukio hilo lilitokea kimakosa kutokana na kufanana kati ya Dk. Ali na gaidi anayesakwa na nchi hiyo.
Dk. Ali alikumbana na kashkash za Wamarekani alipokuwa amekwenda nchini Marekani, katikati ya mwezi Juni mwaka huu akiwa ameambatana na wabunge wengine watano katika msafara uliokuwa ukiongozwa na Waziri Mkuu, Edward Lowassa.