VIONGOZI wa Chama cha Wananchi (CUF) wilayani Magu, wamemshitaki mwanachama na mfadhili wa chama hicho, Manti Chanika, katika mahakama ya wilaya kwa kosa la wizi wa pikipiki aliyokabidhiwa aitengeneze.
Mfadhili huyo, ambaye alikifadhili chama hicho kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu 2005 kwa kuwakopesha fedha za kupangisha chumba cha ofisi, alizungumza na gazeti hili jana na kukiri kushitakiwa na uongozi wa chama hicho.
Alisema kuwa Novemba 22, 2005 alikabidhiwa pikipiki hiyo iliyopata ajali ili aitengeneze, kwa makubaliano ya kurejeshewa fedha zake baada ya uchaguzi, lakini hadi kufikia sasa hajalipwa fedha hizo na badala yake ameshitakiwa mahakamani kwa kosa la kuiba pikipiki hiyo aina ya Honda yenye namba za usajili T 646 AGM.
“Pikipiki hiyo ilipata ajali na kuharibika vibaya sana Septemba 28, 2005 ikiwa katika shughuli za kazi za chama na ilikuwa ikiendeshwa na Kenedy Shelali, hadi kufikia mwezi Novemba chama hakikuwa na fedha za kuitengeneza ndipo waliponiomba niweze kuitengeneza kwa fedha zangu,” alisema Chanika na kuongeza kuwa chama kingemrejeshea fedha zake baada ya kupata fedha.
Kwa mujibu wa barua ya makabidhiano ya pikipiki hiyo yenye Kumb. Na. CUF/MG/92/W/17/008 ya 22/11/2005, Katibu wa Wilaya wa CUF, Francis Mashauri, alisema kuwa: “Baada ya matengenezo gharama zote zitajumuishwa na kulipwa na ofisi (W) na pikipiki kukabidhiwa ofisini.”
Francis amesema kuwa kisa cha chama hicho kumshitaki mfadhili wao huyo kimetokana na yeye (Chanika) kuitumia pikipiki hiyo kama kitega uchumi, kinyume cha makubaliano.
Amesema kuwa ingawa chama hakijapata fedha za kumrejeshea, lakini hakustahili kuitumia pikipiki hiyo kama daladala