JESHI la Polisi nchini, limetoa mwezi mmoja kwa mawaziri, wabunge na maofisa wengine wa serikali,kupeleka silaha wanazomiliki katika jeshi hilo ili zihakikiwe.
Akizungumza na waandishi wa habari katika Makao Makuu ya Jeshi hilo, Dar es Salaam jana, Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi, Dominic Hayuma, alisema muda huo kwa viongozi hao umesogezwa mbele kutokana na wengi wao kuwa Dodoma katika vikao vya Bunge.
“Tumetoa mwezi mmoja kwa waheshimiwa hawa kwani wengi wako Dodoma wakiendelea na kikao cha Bunge, hivyo hawatakuwa na muda mzuri wa kuleta silaha zao ili zihakikiwe kwa muda ambao tumepanga kuanza kazi hii kwa nchi nzima,” alisema Hayuma.
Alisema muda uliopangwa kwa wamiliki wote wa silaha kuanza kuhakikiwa ni Agosti mosi hadi 30.
Alisema jeshi limeanza kutunza kumbukumbu za silaha kwa kutumia kompyuta.
Uamuzi huo ni hatua ya kukidhi matakwa ya itifaki za silaha kwa nchi za Maziwa Makuu na Pembe ya Afrika na ya Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC).
Alisema wamiliki wa silaha wanapaswa kufika kwenye vituo vya polisi wakiwa na nyaraka na silaha itakayohakikiwa, kitabu cha bunduki na leseni aliyolipia bunduki hiyo, picha tatu za paspoti, ada ambazo hazijalipwa na barua ya utambulisho kutoka kwa kiongozi wa mtaa au kijiji anachoishi mmiliki.
Alisema uhakiki huo pia utagusa kampuni binafisi za ulinzi.
Kamishina huyo alisema mmiliki asiyehitaji kuendelea kumiliki silaha, anaweza kuisalimisha kwa Ofisa wa Silaha wa Wilaya.
Alisema miongoni mwa silaha ambazo hazitahakikiwa kwa kipindi hiki, ni pamoja na magobore, kwa madai kwamba silaha hizo zitashughulikiwa baada ya sheria mpya kuanza kutumika.
Aliwataka wananchi walioko vijijini kwenda makao makuu ya wilaya wanakoishi ili kuwa rahisi kuhakikiwa.
Alisema silaha 86,000 nchini kote zinapaswa kuhakikiwa.
“Kumbukumbu zetu zinaonyesha kuna silaha 86,000, takwimu zetu za utunzaji zinaonyesha wapo wamiliki wengi hawalipi kwa wakati unaofaa, hivyo upungufu huu tunataka kuuondoa kabisa,” alisema Kamishina Hayuma.