WATU wanaodhaniwa kuwa majambazi, wamevamia basi lililosheheni watalii wilayani Siha na kuwapora mali na fedha taslimu.
Tukio hilo lilitokea jana mchana wakati watalii hao wakienda kutoa msaada katika Kanisa la International Evangelical lililopo Engale Nairobi wilayani Siha.
Watuhumiwa hao wa ujambazi walitumia pikipiki katika uporaji huo.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Hai, Daniel Sandewa, alizungumza na Tanzania Daima kwa simu na kuthibitisha kuwapo kwa tukio hilo.
Alisema RCO wa Mkoa wa Kilimanjaro, Hezron Kigonda, hadi jana jioni, alikuwa eneo la tukio, akiongoza operesheni ya kuwasaka watuhumiwa hao.
Alisema pamoja na pesa, vitu vingine vilivyoporwa ni kamera, simu selula na zawadi mbalimbali zilizokuwa zikipelekwa katika kanisa hilo.
Habari zilizopatikana baadaye zilisema baada ya uporaji huo, watuhumiwa walijificha katika msitu wa West Kilimanjaro.
Polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), walipelekwa eneo hilo kwa kazi moja ya kuwasaka na kuwanasa majambazi hao.