MAJI yameanza kukauka na samaki hawapatikani tena katika Bwawa la Kyarano, lililojengwa kwa usimamizi wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, na kuhudumia moja kwa moja vijiji vya Butiama, Rwamkoma na Masaba mkoani Mara.
Kukauka kwa bwawa hilo kumetokana na wachimba dhahabu katika mgodi wa Buhemba, kuchukua maji kwa ajili ya shughuli za mgodi wao.
Awali, wananchi walikataa katakata kuutambua mkataba uliosainiwa kati ya viongozi wa mgodi huo na baadhi ya viongozi wa vijiji. Mkataba huo una sifa zote zinazofanana na ule uliosainiwa na Chifu Mangungo wa Msovero na Serikali ya Wajerumani. Akauza nchi kwa kupewa shanga.
Aliyekuwa Waziri wa Maji na Maendeleo ya Mifugo, Edward Lowassa, alisikia kilio cha wanavijiji hao. Akafika Kyarano, akapiga ‘stop’ mkataba huo, lakini katika hali ya kustaajabisha, uamuzi huo ulitenguliwa na uongozi wa juu serikalini.
Serikali ya Awamu ya Nne, chini ya Waziri wa Maji, Stephen Wassira, imerejea kwenye kilio cha wananchi, hasa baada ya kubainika kuwa bwawa hilo lililojengwa mwanzoni mwa miaka ya 1980, sasa linakauka.
Wassira ameuagiza uongozi wa mgodi wa Buhemba utafute haraka chanzo kingine cha maji badala ya kuendelea kutumia maji ya Kyarano.
Akizungumza na Tanzania Daima ofisini kwake juzi, Wassira, alisema serikali imefikia uamuzi huo ili kulinusuru bwawa hilo ambalo lilijengwa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji.
“Tumeuagiza uongozi wa mgodi wa Buhemba kuhakikisha wanatafuta haraka chanzo kingine cha maji, badala ya kuendelea kutumia maji ya Kyarano kwani kina chake sasa kiko hatarini kutoweka na kamwe hatuwezi kuruhusu bwawa lile likauke, lina historia ndefu,” alisema Waziri Wassira.
Alisema kiasi cha maji kinachochukuliwa na mgodi huo kwa siku ni kikubwa, huku kukiwa hakuna jitihada zozote zinazofanywa na wahusika za kulinusuru.
Aliutaka uongozi huo kutafuta njia mbadala ya kuvuta maji kutoka Mto Mara ambao uko umbali wa kilometa 25 hadi mgodini.
“Tumewashauri kwa undani sana, kwamba wafanye kila linalowezekana wavute maji kutoka Mto Mara kwani maji yake ni ya uhakika, hayakauki, umbali wake ni karibu kilometa 25; ni jambo ambalo linawezekana,” alisema Waziri Wassira.
Alisema wananchi pia wanalalamikia uongozi wa mgodi huo kwa kushindwa kukamilisha ahadi walizotoa.
“Eneo lile lina wapiga kura wetu ambao kwa kipindi kirefu wamekuwa wakitoa malalamiko ya kutotendewa haki na uongozi wa mgodi, ikiwa ni pamoja na kulalamika kuharibiwa kwa vyanzo vya maji,” alisema Waziri Wassira.
Alisema ili kukabiliana na tatizo hilo, tayari wizara yake imeunda timu ya wataalamu wanaoondoka Dar es Salaam wakati wowote kuanzia sasa kwenda Musoma kushughulikia suala hilo.
Katika hatua nyingine, Wassira alisema mkataba uliosainiwa na vijiji vinavyomiliki bwawa hilo haukuzingatia athari ambazo zingeweza kutokea kama ilivyo sasa.
“Naamini vingozi waliosaini mkataba ule na uongozi wa mgodi hawakufanya tathimini ya kina kujua uwezo wa bwawa unaweza kuhudumia kwa kipindi gani, sasa hili tutalishughulikia kwa mujibu wa kanuni zilizopo,” alisema Waziri Wassira.