HALI ya mgonjwa aliyepigwa na wawekezaji Wapakistani katika Kiwanda cha Nguo cha NIDA, cha Dar es Salaam ni mbaya.
Mgonjwa huyo, Adinani Khalifa (26), ambaye amelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MHN), wodi ya Mwaisela, anasumbuliwa na tatizo la kutokwa mkojo mfululizo pamoja na maumivu ya nyonga ya mguu wa kushoto.
Hali ya mgonjwa huyo ilidhihirika kuwa ni mbaya jana baada ya Hakimu Mkazi wa Kisutu, Eddy Lyamuya, akiongozana na Mwendesha Mashitaka, Charles Kenyela, kwenda kumwona Muhimbili ili atoe uamuzi wa kuwapa au kuwanyima dhamana watuhumiwa hao, raia wa Pakistan.
Mbali ya kutembelea Hospitali ya Muhimbili kuona hali ya majeruhi aliyepigwa, mahakama hiyo pia ilikwenda katika Zahanati ya Apollo Medical Center iliyopo Mtaa wa Mshihiri, Barabara ya Morogoro kumsomea mashitaka mtuhumiwa, Inamu Shamrey Khani (25), ambaye anasumbuliwa na ugonjwa wa shinikizo la damu kutokana na mshituko wa kutiwa mbaroni kwa tuhuma za kumpiga Khalifa.
Khani ni mkuu wa umaliziaji katika uzalishaji kiwandani hapo na amelazwa tangu juzi, na jana alisomewa mashitaka mawili, la kwanza la kumpiga kwa kutumia kipande cha chuma na kumsababishia maumivu Khalifa, na shitaka la pili ni la kumvunja nyonga na kumsababishia maumivu ya jicho la upande wa kushoto na kumfungia ndani ya kontena.
Katika kesi hiyo watuhumiwa wanadai hawajui lugha yoyote ila Kipakistani, hivyo wanatumia mkalimani kupata mawasiliano mahakamani.
Lakini baada ya mahojiano na mgonjwa Adinani, ilidaiwa kuwa, watuhumiwa wanajua lugha nyingine ikiwa ni pamoja na Kiswahili, Kiingereza na Kipakistani, hata wakati wakimpiga walikuwa wana mtukana matusi kwa lugha ya Kiswahili.
Katika kesi hiyo iliyoanza kusikilizwa juzi, watuhumiwa ni Habibu Khani (30), afisa masoko, Mohamed Rashid (25), mtunza stooo, Shazad Hassani Khani (36), Inamu Shamrey Khani (25), mkuu wa kitengo cha uzalishaji na Mohamed Khalifa (30), mwendesha mitambo.
Watuhumiwa hao wanaongozwa na wakili Justinian Lyabato, ambaye aliwaombea dhamana lakini mahakama ilikataa ombi hilo kutokana na hali ya mgonjwa kuwa mbaya.