Na Mwandishi Wetu
WAZIRI Mkuu, Edward Lowassa, amewaagiza viongozi wa halmashauri za miji nchini kusimamisha semina za maboresho, na nguvu zote zielekezwe katika kuinua kilimo ndani ya maeneo yao.
Lowassa alitamka hayo jana katika majumuisho ya mkutano wa wadau wa kahawa nchini uliofanyika katika ukumbi wa Karimjee, Dar es Salaam, ambao pia ulikuwa ni hitimisho la mikutano ya wadau wa mazao ya kilimo iliyofanyika kwa wiki moja.
Mikutano mingine ilihusisha mazao ya korosho (Ijumaa), pamba (Jumatatu) na juzi ulikuwa wa tumbaku.
“Wakurugenzi (wa halmashauri), madiwani na maofisa wa watendaji wa kata, nasema semina za maboresho sasa basi, sana sana pawepo na ulazima mkubwa,” alisema Lowassa na kuongeza:
“Wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa, sasa fanikisheni kilimo kama mlivyofanikisha ujenzi wa madarasa ya sekondari. Sitaki visingizio, katibu kata kafanya hivi na vile, wote hawa wako chini yenu. Tuanzie hapo, atakayeshindwa tutajua mbele ya safari tutafanya nini.”
Katika mkutano huo, Lowassa aliagiza ifanyike mikakati ya kuongeza uzalishaji wa kahawa nchini kufikia tani 120, 000 ifikapo mwaka 2010, kutoka tani 54,000 za sasa kwa mwaka. Malengo ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika yaliyosomwa awali na Waziri wa Kilimo na Chakula, Joseph Mungai, ni kuzalisha tani 100,000 katika kipindi hicho.
Kuhusu suala la soko, Waziri Mkuu aliagiza wananchi wahamasishwe kuwa na tabia ya kunywa kahawa, baada ya Mungai kusema kuwa soko lake nchini ni dogo mno.
Mungai alisema kuwa serikali imewekeza kiwango kikubwa cha pesa katika kilimo cha kahawa, jambo ambalo litasaidia kupunguza makali ya gharama za uzalishaji kwa mkulima na kumpatia faida kubwa.
Pia waziri huyo alizitaka halmashauri kupunguza kodi za mazao, jambo ambalo nalo litampa unafuu katika uzalishaji wake.
Waziri Mkuu aliitaka wizara inayohusika na kilimo na wadau wengine kuangalia namna ya kusimamia bei ya zao hilo, ili kufikia lengo la kahawa anayoizalisha mkulima ifikie walau asilimia 70 ya soko la dunia.
Akichangia mada, Waziri wa Miundombinu na mbunge wa Rombo, Basil Mramba, aliyejitambulisha kama mkulima mdogo, alisema kuwa tatizo la uzalishaji mdogo wa kahawa ni kutokana na mibuni iliyozeeka ambayo inazalisha asilimia 20 ya uwezo halisi.
Mramba alisema uamuzi mgumu wanaoupata wazalishaji wa kahawa ni iwapo watang’oa mibuni na ndani ya miaka mitano wakati inakua, watakula nini.