Na Selina Wilson, Kibaha
WANANCHI wameacha kuchangia ujenzi wa kituo cha polisi kwa kuhofia watoto wao watawekwa ndani kitakapokamilika.
Ujenzi wa Kituo cha Polisi cha Mwendapole kata ya Kibaha mkoani Pwani umekwama kwa miaka miwili sasa.
Hofu hiyo inatokana na baadhi ya vijana katika eneo hilo kujihusisha na matukio ya uhalifu na kwamba wazazi wao wamekuwa wakiwategemea kuwapatia riziki kutoka na kazi hiyo isiyo halali.
Mwenyekiti wa mtaa wa Mwendapole Mbarouk King`wenyu alisema hayo wakati akizungumza na mwandishi wa habari hii kuhusu maendeleo ya ujenzi wa kituo hicho ambacho ulianza mwaka 2002, na kutarajiwa kukamilika 2004.
Alisema uamuzi wa kujenga kituo hicho ulifanywa na wananchi wenyewe baada ya kukithiri kwa vitendo na matukio ya uhalifu yanayotokea kijijini hapo, hivyo waliona njia pekee ni kuwepo na kituo cha polisi.
King`wenyu alisema matukio mengi ya wizi na uporaji mdogo mdogo yanasababishwa hasa na vijana ambao ni wakazi wa kijiji hicho na baadhi yao hupata upenyo wa kufanya uhalifu kutokana na kukosekana kwa polisi karibu na kijiji hicho.
Alisema baada ya kupitisha uamuzi huo, walikubaliana kila kaya ichangie sh. 300 huku serikali ya mtaa ikiendelea kutafuta wafadhili wa kusaidia ujenzi huo, lakini baadaye mambo yalikuwa kinyume na kaya zilikwama kuchangia na hivyo kuzorotesha ujenzi huo mpaka sasa.
Mwenyekiti alisema hali ya usalama katika mtaa huo haikuwa nzuri, lakini bado wazazi walikuwa wazito kuchangia nguvu zao kujenga kituo na hata sasa tatizo kubwa linasumbua mtaa huo ni uhalifu unaofanywa na vijana wa eneo hilo.
Alisema mpaka sasa kuna baadhi ya vijana wamefungwa jela na wengine bado wanatafutwa huku serikali ya mtaa ikiendelea kudhibiti matukio ya uhalifu kwa kushirikiana na polisi.
Akizungumzia ujenzi wa kituo hicho, alisema umefikia katika hatua ya madirisha na bado kufikia linta na mpaka hapo umegharimu zaidi sh. 500,000 hivyo wameomba wafadhili wajitokeze kusaidia.
Pia, ametoa wito kwa wananchi wa eneo hilo kubadili mawazo ili waendeleze ujenzi huo.