Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti Ukimwi (TACAIDS), Meja Jenerali (Mstaafu) Herman Lupogo, ameiasa jamii ya wafanyabiashara nchini kuwa na sera nzuri za mapambanano dhidi ya Ukimwi makazini ili kulinda nguvu kazi dhidi ya ugonjwa huo.
Meja Jenerali Lupogo aliyasema hayo mwishoni mwa wiki jijini Dar es Salaam kwenye kilele za matembezi ya hisani ya wafanyakazi wa Kampuni ya Sigara Nchini (TCC).
Matembezi hayo yaliandaliwa ili kuchangia fedha kwa ajili ya vita dhidi ya Ukimwi kwa jamaa za wafanyakazi kampuni hiyo.
Alisema ikiwa kampuni yoyote inafanya biashara kwenye jamii iliyozungukwa na ugonjwa huu wa Ukimwi, basi biashara ya pili ya kampuni hiyo ni kupambana na ugonjwa huo ili usijekuiharibu biashara ya kwanza.
’’Nimefurahishwa sana na sera yenu dhidi ya Ukimwi, iko wazi ikilenga kuwakinga wafanyakazi wenu dhidi ya ugonjwa huu?cha muhimu hapa ni kuhakikisha mnayatekeleza haya malengo mazuri yaliyomo humu,’’ alisama Bw. Lupogo.
Bw. Lupogo ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye matembezi hayo ya kilomita tatu, yakianzia makao makuu ya TCC mpaka kwenye klabu ya TCC Chang’ombe alisema ni jambo zuri kwamba wafanyakazi wameamua kuzikumbuka familia zao kwenye elimu dhidi ya Ukimwi kwani ugonjwa huo ni wa jamii nzima.
Alisema ajuavyo yeye ni kwamba yako makampuni mengi yenye kufundisha wafanyakazi wao elimu ya Ukimwi, bado hajaona makampuni yenye kuziingiza familia kwenye elimu ya ugonjwa huo kama walivyofanya TCC.
Kwa upande wake, Bw Da Motta aliishukuru serikali kwa kutambua juhudi za makampuni binafsi za kupambana na Ukimwi.