Watu wanaosadikiwa kuwa ni majambazi, wamemuua mwenzao kwa kumtwanga risasi baada ya kukosea ’mahesabu’ wakati wakiwa katika harakati za kupora kwenye baa moja ya Nonzo Pub, eneo la Mabibo Mpakani, jijini Dar es Salaam.
Kamanda wa Polisi Kanda ya Kinondoni, Bw Jamal Rwambo, alisema tukio hilo lilitokea usiku wa manane wa kuamkia juzi.
Kamanda Rwambo alisema jambazi hilo liliuawa na wenzake kwa kupigwa risasi wakati wakiwa kwenye purukushani za kupora fedha za mauzo ya siku katika baa hiyo.
Akifafanua kuhusiana na mkasa huo, Kamanda Rwambo alisema mmoja wa wateja aliyekuwepo katika baa hiyo, Bw Hamis Chesco maarufu kama Mgata (32), alijeruhiwa vibaya kwa risasi zilizofyatuliwa na majambazi hayo wakati wa tukio hilo.
Alisema majeruhi huyo sasa amelazwa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, akiendelea na matibabu.
Hata hivyo, Kamanda Rwambo alisema majambazi hayo yalifanikiwa kuondoka na kitita cha Sh. 150,000.
Alisema msako mkali wa kuyatafuta majambazi hayo unaendelea na kuwataka wananchi kutoa ushirikiano kwa polisi ili kufanikisha kuwanasa.
Wakati huo huo,mwanamke mmoja Kraine Mfumbi (26), amenyofolewa utumbo wake, baada ya kuchomwa kisu tumboni na mwanamke, anayedaiwa kuwa ni ’nyumba ndogo’ ya mume wake, kutokana na wivu wa mapenzi.
Kamanda wa Polisi wa Kanda ya Ilala, Bw Masindoki Masindoki, alisema tukio hilo lilitokea eneo la Ukonga Mazizini, Gongo la Mboto.
Kamanda Masindoki alimtaja mwanamke aliyemjeruhi kwa kisu kuwa ni Eliza Chilenga (20), ambaye ni mfanyabiashara wa eneo la Mazizini.
Kamanda Masindoki alifafanua kuwa, chanzo cha ugomvi huo ni baada ya Bi. Kraine, ambaye ni mke wa ndoa, kwenda kumuomba mume wake fedha za matumizi, wakati akiwa katika nyumba ndogo hiyo.
Alisema baada ya mke mkubwa kufika katika nyumba hiyo ndogo na kueleza kilichompeleka, mke mdogo alichomoka ghafla kutoka chumbani na kumchoma kisu tumboni, hadi kusababisha utumbo wake kutoka nje ya tumbo.
Ilidaiwa kuwa, mke mkubwa aliamua kumfuata mume wake nyumbani kwa mke mdogo, baada ya kuona amehamia moja kwa na kumtelekeza yeye na watoto wake watatu.
Kamanda Masindoki alisema mtuhumiwa anashikiliwa na polisi na anatarajiwa kufikishwa mahakamani wakati wowote kujibu mashtaka yanayomkabili.