MWENYEKITI wa taifa wa Chama cha NLD, Dk. Emmanuel Makaidi, amesema kupanda kwa mishahara hakutakuwa na maana kama serikali itashindwa kudhibiti upandaji wa gharama za maisha.
Mwenyekiti huyo alitoa maoni hayo jana alipofanya mahojiano maalumu na Tanzania Daima, Dar es Salaam.
“Bajeti hii haimsaidii mwananchi wa kawaida, kwani kupata hiyo shilingi laki moja kisha ukapandisha gharama za umeme, chakula, maji, fedha hiyo haitamudu gharama hizo,” alisema
Alisema bajeti inatakiwa iwe na malengo maalumu kwa kubadilisha maisha kwa watu wenye kipato cha chini kuweza kumudu gharama za msingi na kujiwekea akiba kwa maisha ya baadaye
Aliishauri serikali kutumia mawazo ya wapinzani wenye nia moja ya kuhakikisha kuwa nchi inasonga mbele kimaendeleo.
“Si busara kulaumu serikali kila wakati, tuko tayari kushirikiana na serikali iliyoko madarakani, ikiwa ni pamoja na kushauri pale wanapokwenda,” alisema.
Akizungumzia suala la ruzuku ya sh milioni 500 iliyotolewa kwa kila mkoa kwa lengo la kuondoa umaskini, Dk. Makaidi alisema haitawasaidia kwani ni kiasi kidogo.
“Hizo milioni 500 kwa kila mkoa ni kiini macho, haiwezekani kuondoa umaskini kwa milioni 500 kwa kila mkoa, mtawakopesha watu wangapi?” alihoji Dk. Makaidi.
Alishauri serikali kutenga sh bilioni tano kwa kila mkoa badala ya sh milioni 500 ambazo zitaleta urasimu wakati wa kukopesha.