BARAZA la Maaskofu Tanzania (TEC) sasa lina sura mpya. Lilipata viongozi wapya, akiwamo Rais wake, Askofu Yuda Thadei Ruwa’Ichi wa Jimbo la Dodoma.
Ruwa’Ichi anachukua nafasi ya Askofu Severin Niwemugizi wa Rulenge anayeondoka kutokana na kumaliza muda wake. Askofu Mkuu Norbert Mtega wa Songea, ambaye pia ni Mwenyekiti wa Idara ya Elimu alichaguliwa kuwa Makamu wa Rais.
Katika uongozi huo mpya, yupo Padri Anthony Makunde, anayekuwa Katibu Mtendaji, akichukua nafasi ya Padri Dk. Pius Rutechura, ambaye kwa sasa ana wadhifa wa Katibu Mtendaji wa AMECEA, mwenye ofisi yake jijini Nairobi, Kenya.
Wote hao na wengine ambao ni wenyeviti wa idara mbalimbali, walichaguliwa katika mkutano wa 59 wa TEC. Wenyeviti hao ni Askofu Msaidizi, Dk. Method Kilaini (Fedha na Mipango), Askofu Amedeus Msarakie wa Moshi (Uchungaji), Askofu Jacob Koda wa Same (Utume ), Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa wa Iringa (Liturjia) na Askofu Agapit Ndorobo wa Mahenge (Caritas).
Wengine ni Askofu Aloysius Balina wa Shinyanga (Afya), Askofu Telesphor Mkude wa Morogoro (Katekisi) na Askofu Alfred Maluma wa Njombe (Mawasiliano ya Jamii).
Hiyo ndiyo picha mpya ya uongozi wa TEC, viongozi wake wakitarajiwa kuendeleza mema mengi yaliyoachwa na uongozi uliopita