WAKATI Kamati ya Wazazi katika Shule ya Msingi Buguruni ‘A’, imepiga mbiu ya kutaka wazazi kuchanga sh 3,000 kila mmoja kwa ajili ya madawati, Mratibu wa Elimu wa Kata hiyo, Paulina Nyaki, anadaiwa kutoweka na madawati 11 yenye thamani ya sh 440,000; mali ya shule hiyo.
Habari zilizopatikana zinasema mratibu huyo alichukua madawati hayo Desemba 9, 2003 na hajayarudisha. Kila dawati linagharimu sh 40,000.
Mwalimu Mkuu wa Shule hiyo, Khadija Telela, na Mratibu huyo, hawana maelezo ya wazi kuhusu madawati hayo.
Anadaiwa kuchukua madawati hayo baada ya kueleza kwamba alikubaliwa na Mwalimu Telela.
Tanzania Daima ina ‘memo’ inayoonyesha mwalimu huyo akikubali madawati hayo yachukuliwe na mratibu.
Mlinzi wa shule hiyo alimwandikia barua Ofisa Elimu wa Wilaya, Juni 19, mwaka huu, kuelezea suala hilo, lakini hajapata jibu.
“Katika kikao cha wazazi hivi karibuni wamewataka wazazi kuchanga sh 3,000 kwa kila mtoto kwa ajili ya ununuzi wa madawati, haya mengine yako wapi?” alihoji mlinzi huyo.
Nyaki, alikiri kuchukua madawati hayo, lakini alisema hakumbuki iwapo yaliisharudishwa au la.
“Kwa kweli nilichukua, ilikuwa kwa shughuli yangu binafsi, niliwaagiza watu wayarudishe, lakini sina hakika kama walifanya hivyo,” alisema.
Aliongeza: “Nipe muda nifuatilie, lakini nakumbuka niliagiza yarudishwe, ngoja nitakupigia kukufahamisha.”