Rais Jakaya Kikwete, jana aliwaongoza maelfu ya waombolezaji kuuaga mwili wa aliyekuwa Mhadhiri Mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Sehemu ya Mlimani, Profesa Seith Chachage (51), aliyefariki dunia mwishoni mwa wiki iliyopita.
Rais Kikwete ambaye alitokea nchini Afrika Kusini, alikwenda moja kwa moja hadi kwenye ukumbi wa Nkrumah, ambako mwili wa Profesa Chachage uliagwa.
Rais Kikwete akiwa ameongozana na Mkewe, Mama Salma Kikwete,
kwa pamoja waliweka shada la maua katika jeneza la marehemu Profesa Chachage.
Pia, Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Dk. Asha-Rose Migiro, Waziri Mkuu mstaafu, Joseph Warioba, viongozi wa vyama vya siasa akiwemo Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba, Wabunge, wawakilishi wa taasisi za elimu ya juu nchini na watu mbalimbali mashuhuri.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Matthew Luhanga, wahadhiri mbalimbali na wanajumuiya wa chuo hicho, walikuwepo kutoa salamu zao za mwisho.
Mwili wa marehemu Profesa Chachage, ulisafirishwa jana jioni kwenda kijijini kwake Mtwango, Wilaya ya Njombe, mkoani Iringa kwa mazishi.
Profesa Chachage, alifariki dunia akiwa katika shughuli za kikazi mjini Kibaha, mkoani Pwani.
Hadi kifo chake, Profesa Chachage ambaye alishiriki kikamilifu kwenye mijadala mbalimbali ya kijamii na kisiasa, alikuwa Mwenyekiti wa Wahadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Mkuu wa Kitivo cha Sosiolojia (Sociology) chuoni hapo.
Marehemu Profesa Chachage, alizaliwa mwaka 1955, katika kijiji cha Mtwango, Wilaya ya Njombe, mkoani Iringa.
Alijiuga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kupata Shahada ya kwanza ya Sosiolojia mwaka 1982 na kuajiriwa chuoni hapo akiwa kama Mhadhiri Mwanafunzi hadi mwaka 1983.
Hata hivyo, mwaka huo huo (1983), Profesa Chachage alitunukiwa Shahada ya Uzamili wa Sosiolojia katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na baadaye alijiendeleza zaidi katika Chuo Kikuu cha Glasgow, nchini Uingereza ambako alitunukiwa Shahada ya Juu ya Udaktari wa Falsafa ya Sosiolojia (PhD).
Alitunukiwa kuwa Profesa kamili na UDSM mwaka 2003, baada ya kuwa Profesa Mshiriki katika Chuo Kikuu cha Cape Town, Afrika Kusini mwaka 2000.Marehemu ameacha mjane na watoto watano.