Ndege ya kubeba mizigo inayomilikiwa na Umoja wa Mataifa (UN), ikiwa na askari watano, imeanguka na kuwaka moto mkoani Kigoma. Ilidondoka wakati ikijaribu kutua katika Uwanja wa Ndege wa mjini Kigoma.
Hata hivyo, askari wote, walinusurika kifo baada ya kuruka kutoka ndani ya ndege hiyo, kwa kutumia miavuli.
Meneja wa Uwanja wa Ndege wa Kigoma, Bw. Elipid Tesha, alisema ndege hiyo ilikuwa ikitoka mjini Bunia katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) kuja mjini hapa.
Bw Tesha alisema baada ya askari hao kubaini hatari katika ndege hiyo, yenye namba UN 822, C 130 iliyotengenezwa nchini Urusi, waliamua kuruka kwa kutumia miavuli ili kuokoa maisha yao, huku wakiiacha ikiendelea kuwaka moto.
Alisema ajali hiyo ilitokea jana saa 10:00 jioni.
Bw Tesha alifafanua kuwa, ndege hiyo ina uwezo wa kubeba tani 30 za mizigo.
Lakini wakati wa tukio hilo, haikuwa imebeba mizigo.
Alisema baada ya ndege hiyo kuanguka, iliteketea kabisa kwa moto, baada ya juhudi za kutaka kuuzima kushindikana.
Kwa mujibu wa Meneja huyo, ndege hiyo ilikuwa inakuja Kigoma kufuata chakula na matunda kupeleka Bunia, DRC.