Na Khatib Suleiman, Zanzibar
WAFANYAKAZI wanne wa shirika la umeme la Zanzibar, wakiwemo wanawake wawili, wamefikishwa katika mahakama tofauti wakikabiliwa na tuhuma za kulihujumu Shirika la Umeme pamoja na kuliibia zaidi ya sh. milioni 500.
Watuhumiwa walisomewa mashitaka tofauti ya wizi wa fedha ambapo Leluu Abdalla (48) anatuhumiwa kuiba sh. 25,385,693, wakati Ahmed Hamid Fatawi (38) anadaiwa kukwapua sh. 17,225,604.
Wengine ni Mohamed Abdalla Mohamed (43) aanayekabiliwa na tuhuma za kuliibia shirika sh. 491,667,986 na Fatma Bakari Omar anayedaiwa kuiba sh.2,636,875.
Watuhumiwa wote hao walishindwa kukamilisha masharti ya dhamana ambazo zipo wazi baada ya kutakiwa kulipa sh.milioni 10 kila mmoja, na kulipa sh. milioni moja fedha taslimu pamoja na kuwasilisha hati ya mali isiyohamishika.
Kesi zitatajwa tena Julai 25, mwaka huu. Hata hivyo haikuweza kufahamika mara moja kitakachowasibu washitakiwa wengine wa shirika hilo ambao walikuwa wakishikiliwa katika vituo tofauti vya Polisi tangu kukamatwa wiki iliyopita kufuatia ripoti ya Bodi ya Shirika la Umeme kuwataja kwamba wanahusika na upotevu mkubwa wa fedha.