Na Bashir Nkoromo
KATIBU Mkuu wa CCM mstaafu, Rashidi Kawawa amesema yeye binafsi na wana-CCM wana matumaini na Katibu Mkuu mpya wa chama, Yussuf Makamba, kuwa atakiongoza Chama Cha Mapinduzi kwa umahiri mkubwa.
Mzee Kawawa, ambaye ni muasisi wa chama, alisema hayo alipoungana na viongozi wa chama na serikali mikoa ya Dar es Salaam na Pwani kumpokea Makamba, eneo la Kiluvya jana.
Makamba aliwasili Kiluvya saa 9. 58 alasiri akitokea Tanga ambako alikuwa na ziara ya kikazi ya siku sita, ya kwanza tangu ateuliwe kuwa Katibu Mkuu wa CCM mwishoni mwa mwezi uliopita.
Mzee Kawawa alisema, yeye na wanachama wana imani naye kwa sababu Makamba ni kiongozi ambaye amekuwa akifanya kazi za chama vizuri na kwa uadilifu kwa muda mrefu, hivyo anakifahamu vizuri chama na malengo yake.
"Wewe ni mwenzetu siku nyingi, tunaujua uchapakazi na uadilifu wako katika chama, tuna matumaini makubwa na wewe," alisema na kuongeza: "Sasa chama ni kikubwa na kinafaa sasa kuongozwa na wewe."
Akizungumza kwenye mapokezi hayo, Makamba alisema hatua aliyofikia ni matunda ya Mzee Kawawa kwa kuwa alimpa malezi mazuri kichama, hasa miaka ya 1970 akiwa katibu Mkuu wa CCM.
Makamba alisema, ameshukuru kupata mapokezi makubwa kiasi kile, lakini akaeleza kwamba kimsingi aliyepolewa si yeye, bali kimepokewa chama.
Alisema, ili kudhihirisha kuwa wanachama wanathibitisha kwa dhati kuwa yeye ndiye njia katika chama, wamuunge mkono kwa kuhakikisha wanakuwa hai kwa kulipia ada za uanachama.
Makamba aliwataka wanachama kote nchini kuwa kama waliozaliwa upya na kuimarisha zaidi chama kwa kufuata falsafa ya Mwenyekiti wa Chama, Rais Jakaya Kikwete ya Ari Mpya, Nguvu Mpya na Kasi Mpya.
Alisema CCM ni chama cha wanyonge, wakulima na wafanyakazi, hivyo lazima kujishughulisha na utatuzi wa kero na umasikini wa watu.
Katibu Mkuu aliwaasa wananchi ambao hawajajiunga na CCM kujiunga haraka iwezekanavyo kwa kuwa ndicho chama pekee chenye uhakika wa kushughulikia kero.
"Wananchi sasa jiungeni na chama hiki kwa sababu ndicho chama tawala chenye uwezo wa kushughulikia kero zenu... msikimbilie upinzani mtapoteza muda wenu bure," alieleza.
Aliwataka wananchi wasidanganyike kwenda upinzani akiwatanabahisha kwamba kuchagua kujiunga na CCM ni kuchagua amani, maendeleo na mahala maalum pa utatuzi wa kero zao.
Makamba aliwashukuru wananchi na viongozi aliokuwa akifanya nao kazi akiwa mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam.
"... Enyi wa Dar es Salaam, sitawasahau... nitakuwa nanyi katika ufalme wangu... wale niliowakosea kwa namna moja au nyingine naomba mnisamehe," alisema Makamba.
Aliwataka viongozi na wananchi mkoani kumpa ushirikiano wa dhati Mkuu mpya wa mkoa wa Dar es Salaam, Abbas Kandoro ambaye amechukua nafasi yake.
Pamoja na Kawawa, viongozi waliofika kumlaki Makamba, kwa Dar es Salaam ni pamoja na Mwenyekiti wa CCM mkoa, Hemedi Mkali, Katibu wa CCM mkoa huo, Mattson Chizi, wenyeviti na makatibu wa chama wilaya zote wakati viongozi wa mkoa wa Pwani waliongozwa na Katibu wa CCM, Amina Makilage.
Baadaye msafara mkubwa ulitoka Kiluvya na kumsindikiza Makamba hadi nyumbani kwake mtaa wa Luthuri.
Wakati huohuo, ziara ya Katibu wa uenezi wa Chama Cha Mapinduzim Aggrey Mwanri, iliyokuwa ianze leo mkoani Kilimanjaro imeahirishwa kutokana na majukumu mengine ya kikazi anayotakiwa kuyafanya