Wanatuhumiwa kwa ubadhirifu wa mamilioni
Na Khatib Suleiman, Zanzibar
MAOFISA 11 wa Shirika la Umeme Zanzibar watapandishwa kizimbani leo kwa mashitaka ya ubadhirifu na upotevu wa fedha za shirika.
Watakaofikishwa mahakamani ni pamoja na maofisa wa Idara za Fedha na Uhandisi, kwa mujibu wa Naibu Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai Ramadhan Kinyogo.
Kinyogo alithibitisha kufikishwa kwa wafanyakazi hao
ambao wanashikiliwa na Polisi kwa muda wa siku tatu sasa kwa tuhuma mbali mbali.
Miongoni mwa watendaji wa juu waliokamatwa na ambao majina yao yametajwa kuwa watafikishwa mahakamani ni pamoja na wale wa Idara ya Fedha na Utawala akiwemo Meneja wa Fedha Juma Ahmed, Mhandisi Simai Manzi, Ame Fatwi, Juma Hija, Ali Bushiri, Kassim Bia, Haina Idarous na Thabit Mohamed.
Watumishi hao ambao wanashikiliwa na Polisi tangu mwishoni mwa wiki walikamatwa na polisi katika Makao Makuu ya Shirika la Umeme Gulioni kufuatia ripoti ya Tume iliyoundwa kuchunguza tuhuma za ubadhirifu na upotevu wa mali katika shirika hilo.
“Tunatazamia kuwafikisha mahakamani Jumatatu (leo) baada ya kukamilisha uchunguzi wa mashtaka yanayowakabili sambamba na kusoma ripoti ya uchunguzi wa Tume,” alisema Kinyogo.
Zimekuwepo shutuma mbalimbali kwa muda mrefu za ubadhirifu mkubwa wa fedha kufuatia manunuzi hewa kwa bidhaa mbalimbali
zinazonunuliwa huku nyengine zikiwa hazina ubora unaokubalika ikiwemo vifaa vya transfoma.
Hatua hiyo iliwafanya wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kuishinikiza serikali kuunda Tume kuchunguza ubadhirifu huo ambapo kwa mujibu wa Waziri wa Maji, Ujenzi Nishati na Ardhi Mansour Yussuf Himid alisema shirika linapoteza sh. bilioni moja kwa mwaka.
Fedha hizo hupotea kupitia uunganishaji wa umeme unaofanywa kwa kushirikiana na mafundi wa Shirika la Umeme kinyume cha sheria na hivyo kuliingiza shirika katika hasara kubwa, sambamba na kufanya udanganyifu wa kusoma mita katika hoteli kubwa za kitalii.
Tume hiyo iliundwa baada ya Waziri Kiongozi kutaka kufanyika kwa uchunguzi kufuatia kuwepo kwa taarifa za upotevu mkubwa wa fedha pamoja na ununuzi wa bidhaa hewa unaofanywa na maofisa wakubwa wa shirika hilo.
Tayari aliyekuwa meneja mkuu wa shirika hilo, Suleiman Ali Juma ametimuliwa baada ya kuhusishwa na tuhuma mbalimbali. Hata hivyo, hayumo miongoni mwa maofisa wa waliokamatwa hadi sasa kutokana na tuhuma hizo.