Makamu wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein amelishukuru Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) kwa misaada yake kwa Tanzania ambayo imesaidia kufanikisha jitihada za serikali katika kuwaletea maendeleo wananchi wake.
Dk. Shein alitoa shukrani hizo wakati alipokutana na Mwakilishi Mkazi wa UNDP anayemaliza muda wake nchini, Bw. John Hendra alipokwenda nyumbani kwake Oysterbay kwa ajili ya kumuaga.
Makamu wa Rais alisema Tanzania ina mategemeo makubwa ya kuendelea kufanya kazi pamoja na UNDP na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa katika kuleta mabadiliko katika kilimo, uvuvi na kufanikisha Mpango mzima wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umaskini (MKUKUTA).
Katika mazungumzo hayo, Bw. Hendra ambaye pia alikuwa Mratibu wa Mashirika ya Umoja wa Mataifa nchini alielezea kufurahishwa kwake na ushirikiano alioupata Tanzania katika kipindi chote alichokuweko nchini.
Bw. Hendra alisema pamoja na kwamba anaondoka nchini lakini ameahidi kurudi tena ili kuangalia jinsi Tanzania inavyofanikisha harakati za kuleta maendeleo kwa wananchi.
Bw. Hendra anaondoka nchini leo kwenda kituo chake kipya cha kazi Vietnam ambako ataendelea na nyadhifa alizonazo.
Wakati huo huo, Makamu wa Rais Dk. Ali Mohamed Shein anaondoka nchini leo kwenda Salvador, Brazil, kuhudhuria mkutano wa pili wa wasomi kutoka Bara la Afrika na Ughaibuni.
Makamu wa Rais atamwakilisha Rais Jakaya Kikwete kutokana na mwaliko wa Rais wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva.
Lengo kuu la mkutano huo ni kuangalia uwezekano wa kufufua namna ya kuitumia michango ya wasomi hao kwa ajili ya kupata mawazo mapya, mageuzi ya jamii na maendeleo.
Mkutano huo pia utatoa nafasi kwa mamlaka za serikali, wawakilishi wa vyama vya kiraia na wanafunzi kujadili na wasomi hao juu ya masuala mbalimbali yanayohusiana na umuhimu wa kuimarisha maelewano na maarifa baina ya Afrika na wasomi wa Ughaibuni.
Maudhui ya mkutano huo ambao utafanyika kuanzia Julai 12 hadi 14 ni ’’The diaspora and African Renaissance’’ yaani ’’Watu weusi na kipindi cha mwamko wa waafrika.’’
Akiwa nchini Brazil Makamu wa Rais atakutana na Rais Lula da Silva ambapo watazungumzia umuhimu wa kuimarisha mahusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Brazil.
Katika mkutano huo Dk. Shein atafuatana na mkewe Mwanamwema Shein, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Dk. Mwinyihaji Makame na naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Dk. Cyril Chami.
Viongozi wengine ni pamoja na Mkuu wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Ardhi Prof. Idris Kikula, Mkuu wa Kitivo cha Sheria cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam Prof. Ibrahim Juma na Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya na Amerika kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Balozi Pastor Ngaiza.