MAWAZIRI wawili katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano, wanadaiwa kumkwamisha mwekezaji mzalendo aliyepewa leseni ya kuchimba madini wilayani Ulanga, Morogoro.
Wanaotajwa kuhusika na mpango huo ni Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Celina Kombani; na Waziri wa Mipango, Uchumi na Uwezeshaji, Dk. Juma Ngasongwa.
Mwekezaji huyo mzalendo, anadai kukwamishwa kuwekeza kwenye uchimbaji madini wilayani humo, licha ya kupewa leseni halali kutoka mamlaka zinazohusika.
Wilaya ya Ulanga ina majimbo mawili ya uchaguzi - Ulanga Mashariki (Kombani), na Ulanga Magharibi (Juma Ngasongwa).
Mchimbaji huyo wa madini amelalamika kwamba viongozi hao, kwa kutumia nafasi zao za ubunge, wamehamasisha wananchi wamzuie kuchimba madini katika eneo hilo.
“Nina leseni halali ya kuchimba madini eneo la Ipanko, lakini nimezuiwa na wananchi wanaohamasishwa na mawaziri hao wawili.
“Wanasema siwezi kuchimba madini Ipanko, labda wanionyeshe eneo jingine, lakini siwezi kwenda eneo jingine kwa sababu leseni yangu imenielekeza eneo hilo ambalo nimeshalifanyia utafiti,” alisema.
Mwekezaji mwingine mzalendo alisema ni jambo la hatari kuona kuwa viongozi wakuu wanashiriki kuwahamasisha wananchi kuwakataa wachimbaji wazalendo.
“Hii ni kampuni ya wazalendo, ni ya Watanzania, kwa nini tuzuiwe? Kwani wageni ndio wenye haki ya kutetewa na viongozi?” alihoji mchimbaji huyo.
Kombani jana alizungumza na Tanzania Daima kwa simu kuhusu tuhuma hizo, na kusema hajui lolote kuhusu madai hayo.
“Sina habari, na si kweli kuwa mimi na waziri mwenzangu tunawahamasisha wananchi kupinga kampuni hiyo.
“Siwajui kabisa, Ipanko kuna wawekezaji wengi wanaokuja, nadhani kuna jambo jingine zito zaidi ya hilo, sijawahi kuonana na hao wanaolalamika.
“Siwezi kuhamasisha wananchi wampinge mwekezaji, tena mwekezaji wa ndani, siwezi,” alisema Kombani.
Pamoja na maelezo hayo ya Kombani, uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima umebaini kuwa kuna kundi la vijana wanaohamasishwa kumzuia mwekezaji huyo mzalendo