WAZIRI Mkuu Edward Lowassa, amesema ni aibu kwa mwanaume kuomba chakula kwa mwenzake, wakati aliamua kuoa kwa hiari.
Lowassa alisema kuanzia sasa, serikali haitatoa msaada wa chakula kwa wananchi, badala yake itawasaidia uzalishaji kwa kutoa mbolea na ushauri.
“Ni aibu sana mwanaume kuomba chakula kwa mwanaume mwenzie, wakati yeye mwenyewe aliamua kuoa mke kwa hiari,” alisisitiza.
Aliyasema hayo juzi wilayani Bahi, alipokuwa akikagua ujenzi wa Barabara ya Dodoma – Manyoni, ambayo inatarajiwa kukamilika Septemba, mwaka huu.
Waziri Mkuu alisema kwamba, serikali haiwezi kuwalisha wananchi, na badala yake itasaidia uzalishaji wa chakula kwa wananchi kwa kutoa mbolea na kuwapatia wataalam kwa ajili ya ushauri wa mazao gani yalimwe katika maeneo husika kwa ajili ya uzalishaji wa chakula.
Lowassa alisema katika mwaka huu wa fedha, serikali imetenga ruzuku ya sh bilioni 21 kwa ajili ya kununulia mbolea.
Aliwataka wananchi wa wilaya hiyo mpya, kutumia fursa ya barabara kwa uzalishaji, ambao utawaletea maendeleo katika wilaya yao mpya. Alisema serikali imeitengea wilaya hiyo sh milioni 200 kwa ajili ya ujenzi wake.
Awali akitoa taarifa ya ujenzi wa barabara hiyo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Miundombinu, Mkurugenzi wa Barabara Kuu, Leopard Mujjungi, alisema ujenzi wa barabara hiyo utakamilika Septemba, mwaka huu.
Mujjungi alisema kwamba, mradi huo ambao utagharimu zaidi ya sh bilioni 63.89, mpaka sasa umekamilika kwa kiasi cha asilimia 51, ambapo mkandarasi ambaye ni Kampuni ya Konoike, ameshalipwa sh bilioni 8.79, sawa na asilimia 52 ya malipo, ambayo ni makubwa kuliko kazi iliyofanyika.
Mkurugenzi huyo alisema mradi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 127, haujakamilika kwa asilimia 90 na uko nyuma kwa miezi 12 kutokana na usanifu kuchelewa kwa sababu mbalimbali na kurudiwa mara kwa mara