Na Mohammed Mhina, Jeshi la Polisi, Mwanza
MKUU wa Jeshi la Polisi nchini, Inspekta Jenerali Saidi Mwema, amewagiza makamanda wa Polisi wa Mikoa kupanga haraka askari katika kata ili kushirikiana na wananchi kufanya doria katika maeneo hayo.
IGP Mwema alitoa agizo hilo jana wakati akifungua semina ya siku mbili kwa askari wa ngazi ya chini, madiwani, maofisa watendaji kata, wenyeviti wa serikali za mitaa na vijiji vya Manispaa ya jiji la Mwanza, inayojadili rushwa na mikakati ya kupambana na vitendo vya uhalifu nchini na vita dhidi ya rushwa na ujambazi.
Kutokana na hatua hiyo, IGP amewaomba viongozi wa ngazi ya kata, mitaa na vijiji kuwapa ushirikiano polisi watakaopangwa katika maeneo yao kwa kutoa taarifa zitakazofanyiwa kazi haraka.
Alisema kuwa mikakati ya Jeshi la Polisi ni kutaka kuona ni jinsi gani wananchi wataweza kutoa taarifa za wahalifu na kufanyiwa kazi.
Awali, akimkaribisha Mkuu wa Jeshi la Polisi kufungua semina hiyo, Mkurugenzi wa upelelezi wa makosa ya jinai nchini, Kamishna Robert Manumba, alisema kuwa madhumuni makubwa ya semina hiyo kwa askari wa ngazi ya chini na maofisa wa serikali za mitaa na vijiji ni kutaka kujadili maeneo yanayolalamikiwa na wananchi ili kuona jinsi ya kuyapatia ufumbuzi.
Alisema kuwa washiriki wakuu wa katika semina hiyo ni askari wa ngazi ya chini, wakiwemo wa usalama barabarani, ambao alisema wamekuwa wakilalamikiwa kwa vitendo vya rushwa.
Washiriki wengine ni askari wnaofanya kazi katika vituo vidogo vya polisi, maeneo ambayo pia yanalalamikiwa kuwepo kwa vitendo vya rushwa.
Mkuu huyo wa Jeshi la Polisi pia amemwagiza Mkurugenzi wa Upelelezi wa makosa ya Jinai nchini kuendeleza semina kama hizo katika kanda nyingine ili kutoa elimu kwa askari wa ngazi ya chini na watendaji kata, vijiji na wenyeviti wa serikali za mitaa na vijiji.