NCHI ya Burundi licha ya matatizo iliyonayo kuhusiana na masuala ya usalama, imekuwa nchi ya pili barani Afrika kukubali kupeleka askari wa kulinda amani nchini Somalia.
Hayo yalielezwa jijini hapa juzi na El Ghassim Wane, ambaye ni Mkuu wa Kitengo cha kudhibiti migogoro katika Umoja wa Afrika (AU), katika warsha ya waandishi wa habari kuhusu masuala ya amani barani humu.
Wane alisema Burundi imekubali kupeleka bataliani mbili, ambazo zitakuwa na jumla ya askari 1,700 watakaopelekwa kabla ya mwishoni mwa mwaka huu kukabili hali ya mambo nchini humo.
Askari hao wa Burundi wataungana na askari wa Uganda, waliopelekwa mapema mwaka huu na kufanya idadi ya askari katika kikosi hicho kuwa zaidi kidogo ya 3,000, ambao hata hivyo, ukilinganisha na mahitaji ya askari 8,000, bado wanaonekana ni wachache. "Tumezungumza na nchi nyingi na Burundi imeshakubali kuleta bataliani mbili. Nigeria na Ghana nazo zimeonyesha nia ya kutaka kuleta askari… tunatarajia kuwa azma yetu ya kupeleka kikosi cha kulinda amani nchini Somalia hatimaye itatimia," alisema.
Hivi sasa ni Uganda pekee yenye askari kati ya 1,500 na 1,600 nchini humo ambao walipelekwa kwa ajili ya kazi ya kulinda amani. Askari hao wapo mjini Mogadishu ingawa serikali ya nchi hiyo ina makao yake makuu katika mji wa Baidoa, ambako inalindwa na vikosi vya majeshi ya Ethiopia.
Askari hao wa Uganda wameelezwa kuwa hawafanyi kazi iliyowapeleka, kwani wengi wao wanahusika katika kugawa misaada ya kiutu na si kulinda amani kama ilivyotarajiwa.
Hata hivyo, vikosi hivyo vimekuwa vikikumbana na mashambulizi ya waasi na askari kadhaa wameshauawa katika mashambulizi hayo.
Mbali ya Uganda, Tanzania nayo imejitolea kuwapatia mafunzo maofisa wa kijeshi wa Somalia na inatarajiwa kuwa watakapohitimu mafunzo hayo, maofisa hao watatumika kuwafundisha askari wengine wengi zaidi nchini mwao.
Tanzania imeukubali mpango huo kama sehemu ya kuisaidia Somalia kujenga na kuimarisha taasisi zinazohitajika katika kujitegemea yenyewe katika nyanja ya amani.