KESI ya kuwapiga waandishi wa habari inayowakabili askari magereza, imeanza kusikilizwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam.
Kesi hiyo ilianza kusikilizwa kwa mwandishi wa habari kutoka Kituo cha Kutetea Haki za Binadamu (LHRC), Christopher Kidanka kutoa ushahidi wake.
Akiongozwa na Mwendesha Mashitaka Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Charles Kenyela, Kidanka alidai kuwa yeye na waandishi wenzake walipigwa walipokuwa wanapiga picha katika mgogoro kati ya wakazi wa awali wa nyumba za waliokuwa wafanyakazi wa ATC na askari hao.
Alieleza kuwa, Septemba 9 mwaka jana, saa 5 usiku alipigiwa simu na Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Helen Kijo-Bisimba iliyomtaka siku inayofuata akusanye waandishi wa habari ili waende katika eneo la tukio hilo, Ukonga Madafu.
“Nilifanya kama nilivyoagizwa na mkurugenzi. Waandishi nilioambatana nao ni Mwasu Swale wa Mtanzania, Mpoki Bukuku wa Citizen na Boy Ludovick wa Chanel ten.
“Tulipofika tukaona vyombo vya wafanyakazi wa ATC tayari vimetolewa nje na kulikuwa na lori la magereza likiwa limepakia vyombo vinanyosadikiwa kuwa vya wafanyakazi wa magereza, vikiwa vinaingizwa ndani ya nyumba hizo,” alieleza Kidanka.
Alidai kuwa kutokana na hali hiyo, walianza kupiga picha na ndipo wakatokea askari magereza na kuanza kuwanyang’anya kamera. Alieleza kuwa hali hiyo ndiyo iliyosababisha mvutano mkubwa kati yao na askari hao, mpaka kufikia hatua ya kupigwa na kujeruhiwa.
Kidanka alieleza kuwa, Bukuku alianzwa kupigwa na alipokwenda kumwamulia, ndipo alipotokea askari mmoja ambaye alipiga filimbi na kusababisha askari wengine zaidi ya 50 kufika eneo la tukio na kuwapiga waandishi.
“Walitumia fimbo, virungu na baada ya hapo wakatupakia kwenye Land Rover mpaka sehemu ambayo hatukuifahamu, na ndipo wakasimamisha gari katika jua kali kwa muda wa saa moja, huku damu zikiwa zinatuvuja na kutuongezea maumivu,” alieleza. Kidanka aliwatambua askari magereza wawili waliohusika katika tukio hilo.
Askari aliowatambua ni A.255 Sajenti Charles Kija (47) na A. 8440 CPL Martine Mwakyoma.
Awali, ilidaiwa kuwa Septemba 10 mwaka jana, askari hao waliwapiga na kuwajeruhi waandishi wa habari wawili ambao ni Kidanka na Bukuku.