Kitaifa
   Siasa
   Jamii
   Uchumi
   Makala

 

Search


Advanced Search

 »  Home  »  Habari za Kitaifa  »  Mabalozi waikamata Serikali ya JK pabaya
Mabalozi waikamata Serikali ya JK pabaya
By Marshy Abdu | Published  10/6/2007 | Habari za Kitaifa | Rating:
Mabalozi waikamata Serikali ya JK pabaya
na Tamali Vullu


MSIMAMO wa mashirika na mataifa mbalimbali wa kuitaka serikali kuchunguza tuhuma za ubadhirifu zinazoikabili, zimeonekana dhahiri kuishtua Serikali ya Awamu ya Nne.

Mshtuko huo wa serikali ulidhihirishwa jana na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, muda mfupi baada ya kurejea kutoka kwenye ziara ndefu nchini Marekani, alikokuwa na Rais Jakaya Kikwete.

Waziri Membe, alisema mabalozi hao wapo nchini kwa shughuli za kidiplomasia, na si kujihusisha na masuala ya kisiasa, huku akisisitiza kuwa kufanya hivyo ni uchochezi.

Kauli hiyo ya Membe inakuja siku chache tu baada ya mabalozi wa mataifa makubwa ya Ulaya Magharibi na wawakilishi wa taasisi za fedha za kimataifa kuitaka serikali kuzifanyia kazi tuhuma zote za rushwa dhidi ya viongozi na zile za ubadhirifu katika Benki Kuu.

Membe ambaye alitangaza msimamo wake huo kwa waandishi wa habari jana asubuhi kabla ya kukutana na mabalozi hao jana hiyo hiyo mchana, alisema iwapo mabalozi hao wanakerwa na masuala mbalimbali nchini, wanapaswa kufuata taratibu zao za kazi, kwa kutoa maoni na kuwasilisha kwenye Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa au katika vikao halali.

“Kuna taratibu za mabalozi kutoa maoni yao, si kuzungumza majukwaani. Wanapaswa kufuata taratibu za mkataba wa Vienna…wanatakiwa kutoa maoni yao kwa maandishi wizarani ama katika vikao halali. Sasa wanapozungumza, sijui wanazungumza kwa niaba ya wakubwa wa nchi zao au wao.

“Lakini tulipokuwa katika ziara na Rais Kikwete, viongozi wa huko wamekuwa wakitupongeza kwa juhudi za kupambana na rushwa, lakini huku mabalozi wao wanatulaumu,” alisema.

Waziri huyo alisema katika nchi mbalimbali walizopo mabalozi, watu hawazungumzii masuala kama hayo na iwapo watafanya hivyo watafukuzwa katika nchi hizo kwa kuwa wamevunja sheria.

Alisema, mabalozi hao wanapaswa kufanyia kazi mambo ya kidiplomasia, na kuongeza kuwa atawaeleza suala hilo mabalozi hao atakapokutana nao, kwa kuwa uongozi wake ni imara.

Hata hivyo, alisema wananchi wana haki ya kulalamikia hatua zinapochelewa na si mabalozi.

Aidha, alieleza kuwa ni jambo la kusikitisha kuona kuwa watu wanaishinikiza serikali kuwachukulia hatua watu waliotajwa kuhusika na tuhuma za ufisadi, wakati bado tuhuma hizo zinafanyiwa uchunguzi.

“Huwezi kupambana na suala la rushwa bila kufanya uchunguzi…baada ya tuhuma hizo kutolewa, serikali inafanyia uchunguzi tuhuma hizo na utakapokamilika watakaobainika watachukuliwa hatua stahili kwa kuwajibishwa au kufukuzwa.

“Serikali ya Awamu ya Nne ambayo imedhamiria kupambana na rushwa, haitaweza kukaa kimya bila kuwachukulia hatua watu watakaobainika kujihusisha na ufisadi iwapo uchunguzi utabaini hivyo,” alisema.

Waziri huyo katika kudhihirisha kuwa Rais Kikwete amedhamiria kupambana na rushwa, alisema Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU), imeboreshwa na baadhi ya maofisa wamepelekwa masomoni kujifunza jinsi ya kuchunguza tuhuma za rushwa.

Membe, alitumia nafasi hiyo kuwaomba wananchi waendelee kuwa wavumilivu wakati uchunguzi wa tuhuma hizo unafanyiwa kazi, ili utakapokamilika, Rais Kikwete awachukulie hatua waliobainika.

“Lazima tuwe wavumilivu, ripoti ikiwa tayari na ikifika mezani kwa bwana mkubwa, walengwa watawajibishwa, kwani Serikali ya Awamu ya Nne tumedhamiria kupambana na rushwa…mkiona kuna ucheleweshaji, basi kuna contradiction sehemu, lakini ukiwepo ushahidi, hatua zitachukuliwa,” alisema.

Aidha, katika hatua nyingine, waziri huyo alisema haoni ubaya wa mawaziri kufanya ziara mikoani kuelezea bajeti, na kuongeza kuwa hiyo ndiyo siasa, kwani mpinzani anapokwenda kufukua, chama tawala kinakwenda kufukia.

“…hata mimi kesho nakwenda Arusha kufukia mashimo yaliyoachwa wazi na wapinzani…hii ndiyo siasa. Pia nitakutana na mabalozi kujitetea na kuwakumbusha kufuata miiko yao ya kazi. Sisi ndio tunajua zaidi kuhusu rushwa nchini, hivyo wao hawawezi kutuzungumzia,” alisema.

Alitumia nafasi hiyo pia kuwashauri wapinzani kutafuta hoja ya kwenda nayo katika uchaguzi wa mwaka 2010, kwani tuhuma walizozitoa hazitakuwa na nguvu baada ya watu watakaobainika kuhusika kuchukuliwa hatua.

Wakati huo huo, Waziri Membe, alieleza kuwa ziara ya Rais Kikwete anayetarajiwa kurejea nchini leo, imekuwa ya mafanikio makubwa.


How would you rate the quality of this article?
1 2 3 4 5
Poor Excellent
Add comment
Comments
  • Comment #1 (Posted by Atanaye Kijiko)
    Rating
    Sioni kwanini serikali ishituke-Ari mpya na Kasi mpya ndio ilani ya Awamu ya nne...Labda hao mabalozi wanaona kasi ni ndogo na ari hiyo inawapeleka kusikotakikana, vilevile kama hao mabalozi wamekiuka taratibu, basi wakemewe ipasavyo kama Mh. Bw.Membe alivyodai.
    Watanzania jambo hili siyo jipya ila nafikiri walitaka serikali iipatie kipaumbele ili kuonyesha they are serious na rushwa au ufisadi wa namna hiyo!
     
Submit Comment


Article Options
Popular Articles
  1. Unaifahamu Jambo Forums?
  2. Ghorofa Jijini lanusurika kuungua moto
  3. Britsh M.P. calls for the suspension of aid to Tanzania.
  4. Is Tanzania a safe place to invest?
  5. Nitaendelea kugombea nafasi za kisiasa- Balozi Karume
No popular articles found.
Popular Authors
  1. Habari Tanzania
  2. Mzee Mwanakijiji
  3. Nthelezi Nesaa
  4. Linda Garner
  5. Marshy Abdu
  6. Prosper Kwigize
  7. Salehe Mmoro
  8. Ramadhan Semtawa
  9. Manyerere Jackton
  10. Ndesanjo Macha
No popular authors found.