MWENYEKITI wa Chama cha Tanzania Labour (TLP), Augustine Mrema, amesema leo ataanza kukabidhi baadhi ya mikoba yake kwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto (Chadema), ikiwa ni ishara ya kuanza kustaafu siasa.
Alisema mikoba hiyo atamkabidhi leo jijini Dar es Salaam katika mkutano wa hadhara utakaofanyika Temeke, Dar es Salaam. Mrema alisema hayo alipokuwa akihutubia mkutanbo wa hadhara uliofanyika mjini hapa katika Uwanja wa Shule ya Msingi Sabasaba.
“Kwa hili la kuanza kuachia ngazi, roho yangu nyeupe, jamani awali nilishindwa kuacha mikoba hii kwa kuwa niliokuwa nao hakuna wa kumuachia. Waliokuwepo ambao baadhi yao wamerudi CCM wangeuua upinzani,” alisema Mrema.
Alisema yeye (Mrema) si mnafiki na kueleza kwamba, mtu mnafiki ni yule anayeshindwa kutekeleza ahadi anazozitoa.
Naye Mweyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), aliwaambia Watanzania kuwa katika kutetea masilahi ya walalahoi, hamwogopi kiongozi yeyote katika dola, isipokuwa anawaheshimu.
Alisema leo atakwenda kuonana na Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robart Manumba, kumweleza nia ya vyama vya siasa nchini.
Alisema vyama vya siasa vina nafasi yake kwa wananchi na serikali yenye vyombo vya utumishi, kikiwemo alimo Manumba, inatekeleza mustakabali wa utumishi kwa sheria si kwa matakwa ya chama fulani.
“Ndugu zangu Watanzania, mimi Kamanda Mbowe simuogopi mtu kwa madaraka yake, ila nawaheshimu, nasema nitaendelea kutetea haki za wanyonge tunaopigika bila kosa, ambapo roho yangu nimeitanguliza mbinguni kwa kazi hiyo,” alisema Mbowe.
Aliwasihi viongozi waliopo madarakani, akiwemo DCI Manumba, IGP Said Mwema na Rais Jakaya Kikwete, kutojisahau na kudhani kuwa hapo walipo wamefika na badala yake wakumbuke kuwa ni dhamana ya muda mfupi.
“Watanzania tunasahau hilo na kuanza kupumbazwa na rangi za bendera na kuanza kuwekeana chuki za ajabu na kupigana, kuumizana, hatimaye kuuana kwa tatizo la rangi za bendera, ni ajabu kubwa sana,” alisema.
Alisema uajabu tulionao Watanzania umejionyesha tena pale tunapompuuza Profesa Ibrahim Lipumba, huku dunia ikimtafuta kwenda kuwafanyia kazi.
Naye Zitto aliyekuwa akishangiliwa na watu katika mkutano huo, aliwaambia wakazi wa mjini hapa kuwa, hajutii uamuzi wa kusimamishwa kuhudhuria vikao vya Bunge, isipokuwa uamuzi wa wananchi kuchagua wabunge wengi wa CCM, huku wakifahamu kazi yao kubwa ni kusaka ulaji.
Alisema endapo Bunge lingekuwa na wabunge wengi wa upinzani na imara kutetea masilahi ya wanachi, Tanzania ingenufaika na kuboresha maisha ya Watanzania kupitia katika migodi 17 ya dhahabu nchini, ambayo sasa inaliingizia taifa asilimia 47.8 ya mapato yatokanayo na dhahabu.
“Haya yanafanywa kwa makusudi na ufisadi na utawala wa CCM kwa faida ya matumbo ya wachache waliomo katika utawala huo,” alisema Zitto.
Aliwataka vijana kuongeza ujasiri katika mapambao dhidi ya aliouita ufisadi ndani ya serikali iliyoko madarakani, ambao kama watauachia wataendelea kuwa masikini siku zote.