na Makuburi Ally MECHI ya kusaka tiketi ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kati ya Tanzania, Taifa Stars na Msumbiji iliyopigwa Jumamosi, kwenye uwanja mpya, jijini Dar es Salam, imeingiza sh mil 605.02. Kwa kiasi hicho, mechi mbili zilizochezwa kwenye uwanja huo, yaani ya Septemba Mosi dhidi ya Uganda iliyoingiza sh mil 234 na hii ya Msumbiji, zimeingiza jumla ya sh mil 839. Mechi dhidi ya Uganda, ilikuwa ni ya kujiandaa na mechi ya mwisho dhidi ya Msumbiji. Kwa mujibu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), kiasi cha sh mil 605 za mechi dhidi ya Msumbiji, kimetokana na watazamaji 55,514 walioingia na kushuhudia Stars ikitandikwa 1-0 na Msumbiji. Silas Mwakibinga, ambaye ni Mkurugenzi wa Fedha wa TFF, alisema walioingia kwa upande wa VIP A na kulipa sh 50,000, walikuwa 743, hivyo kuingiza sh 37,150,000. Jukwaa la VIP B lililochukua watu 1,973, zilipatikana sh 78,920,000. Mwakibinga alisema kwa upande wa VIP C, ambako jumla ya watu 2,242 waliingia na kila mmoja kulipa sh 30,000, zilipatikana sh 67,260,000. Jukwaa la Orange Straight, ambako watazamaji walikuwa 5,326 na kila mmoja kulipa sh 20,000, zilipatikana sh 106,520,000. Jukwaa la Orange Curve, kulikokuwa na watu 7,300 na kila mmoja kulipa sh 10,000, zilipatikana sh mil. 73 huku mzunguko wa bluu uliochukua watu 18,340 na kila mmoja kulipa sh 10,000, zilipatikana sh 183,400,000. Mwakibinga, alisema Jukwaa la Green Round, lililochukua watu 19,590 na kila mmoja kulipa sh 3,000, zilipatikana sh 58,770,000. Alisema, kiasi hicho ni asilimia 94 ya lengo lililokuwa limekusudiwa, kwani ilikuwa zipatikane sh 644,530,000. Hata hivyo, hakuna ufafanuzi wowote kuhusu mgawanyo wa mapato hayo, kwani Mwakibinga alipoulizwa hilo, alisema hadi baada ya kamati husika kuketi. Katika hatua nyingine, Rais wa TFF, Leodegar Chilla Tenga, alisema nguvu zote sasa ni kwenye michuano ya awali ya kusaka tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Afrika na Kombe la Dunia zitakazofanyika katika nchi za Angola na Afrika Kusini mwaka 2010. Akizunguma na waandishi wa habari jana, Tenga alisema ili kufikia malengo hayo, inabidi kocha Marcio Maximo aangalie aina ya wachezaji wanaofaa kwa timu ya taifa, mfumo, ufundi, mbinu, afya, ukakamavu, saikolojia na nidhamu. Tenga alisema wachezaji inatakiwa wajione kuwa bado ni wachanga sana kimpira, kwani wasijione kama wameshafika, wanahitajika kufanya bidii zaidi katika mazoezi katika timu zao na timu ya taifa. Aidha, alisema mara baada ya kupokea taarifa ya ufundi kutoka kwa Maximo, TFF itatayarisha awamu ya pili ya mpango wa kuiendeleza Stars kwa kipindi kingine cha miaka miwili ambacho kitakoma mwaka 2009. “Mpango wa sasa ulianza Machi 2006, ambako hadi kambi ya timu ya taifa inavunjwa Jumapili, imefanikiwa kukaa kambini kwa wiki 33,” alisema. Tenga alitoa shukrani kwa mashabiki, wapenzi, wadhamini na Rais Jakaya Kikwete kwa kuonyesha moyo wa kuijali timu ya taifa. |