Jumla ya migogoro 62 imewasilishwa kwa kamati maalumu ya uchunguzi wa migogoro ya ardhi wilayani Kibondo mkoani Kigoma katika kipindi cha mwezi mmoja tangu kuanza kazi kwa kamati hiyo.
Mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kibondo ambaye pia ni mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kibondo Bw. Simon Kanguye ametoa taarifa hiyo mwishoni mwa wiki wakati akitathimini kazi za kamati hiyo maalumu.
Bw. Kanguye ameeleza kuwa kamati hiyo imekuwa ikisafiri katika maeneo yote wilayani kwa kuyagawa katika kanda ambapo wananchi wamepata fursa ya kufikisha malalamiko yao mbele ya kamati hiyo.
Amefafanua kuwa miongoni mwa migogoro ya ardhi iliyoripotiwa ni pamoja na wamiliki wa viwanja kugonganishwa katika kiwanja kimoja zaidi ya wamiliki wawili na migogoro ya mipaka.
Kamati maalumu ya kusikiliza migogoro ya viwanja iliundwa na halamashauri ya wilaya ya Kibondo tangu mei 28 kufuatia agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ambaye alizitaka wilaya zote kuunda kamati ya kufuatilia migogoro ya ardhi.
Bw. Kanguye ameuambia mtandao wa HabariTanzania kuwa mapema wiki ijayo wilaya inatarajia kukamilisha shughuli hiyo ya uchunguzi kwa kutoa taarifa na kufanya taathimini ya uchunguzi wake.
Kamati ya kuchunguza migogoro ya ardhi wilayani Kibondo inaundwa na afisa usalama wa wilaya, afisa wa taasisi ya kupambana na rushwa TAKURU, afisa tawala wa wilaya pamoja na mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya.
Hata hivyo uchunguzi uliofanywa na mwandishi wa habari hii umebaini kuwa walalamikaji wengi huhihitaji migogoro yao itolewe maamuzi haraka na kamati hiyo kutokana na kile kinachodaiwa kuwa kamati inawalinda walalamikiwa kwa kutokuwasimamisha kuendesha shughuli katika viwanja vyenye migogoro.