· Wengi ni sura mpya, mwenyekiti mtetezi aangushwa vibaya
· Vijana wachaguliwa kwa wingi.
Chama cha mapinduzi wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma Jumanne wiki hii kimepata viongozi wapya watakaokiongoza kwa kipindi cha miaka mitano ijayo, huku kikimwacha mtetezi wa nafasi ya uenyekiti.
Katika uchaguzi huo mgombea mtetezi wa nafasi ya mwenyekiti Bw. Kinyota Mjege Kapaya ameangushwa vibaya na wagombea wapya na kuachwa akiambulia kura 47 kati ya kura 940.
Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo msimamizi mkuu wa uchaguzi huo Bw. Simon Kanguye ambaye ni mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kibondo alimtangaza meja mstaafu wa jeshi la wananchi Bw. Clement Ndayeza kuwa mshindi baada ya kujizolea jumla ya kura 574.
Aliyefuata katika matokeo hayo ni mwenyekiti mstaafu wa halmashauri ya wilaya ya Kasulu Bw. Juma Ulimwengu ambaye aliambulia kura 305 kati ya kura 940 ambapo kati ya hizo kura 8 ziliharibika.
Kwa upande wake Bw. Kinyota Kapaya (mstaafu) akisaini hati ya kukubali matokeo alikiri kushindwa na kuwataka wajumbe na wanachama wote wamuunge mkono mwenyekiti mpya na aliahidi kumpa ushirikiano wa dhati endapo utahitajika.
Aidha wajumbe waliochaguliwa kushika nafasi ya ujumbe wa mkutano mkuu wa taifa kutoka wilaya ya Kasulu ni Mkuu wa wilaya hiyo Bw. Said Bwanamdogo, katibu wa UWT wilaya Bibi. Alexandrina Katabi, Felista Pius (karani wa ofisi ya CCM mkoa), diwani wa kata ya Nyakitonto (mwanamke) bibi. Yusta Kayagula na mwenyekiti wa halmashauri ya wilaya ya Kasulu Bw. William Luturi.
Nafasi za makundi kuingia katika halmashauri kuu ya wilaya kutoka kundi la jumuia ya umoja wa vijana UVCCM zilishikiriwa na Prosper Kwigize mwandishi wa habari, Adela Sunzu, Masoud Kitowe na Meshaki kalimanzila.
Kundi la UWT kuingia halmashauri kuu walipata nafasi Bi. Amina Nyange, Pili Buyogera, Bi. Froliana Ntikahavuye (afisa elimu wilaya) na Getruda Kanyerere, wakati kutoka kundi la wazazi waliibuka washindi wawili Bw. Elisha Bagwanya na Bw. Abdallah Ntahuga.
Nafasi ya mkutano mkuu wa mkoa ilishikiriwa na Getruda Kanyerere na Bw. Alex Mbonankira wakati katibu wa itikadi na uenezi alichaguliwa Bw. Meshack Kalimanzila na katibu wa uchumi na fedha alichaguliwa Bw. Deusdedit Kibabi.
Wajumbe watano wa kamati ya siasa waliochaguliwa na mkutano wa halmashauri kuu ya CCM wilaya ni Mwandishi wa habari wa Radio Kwizera Bw. Prosper Kwigize, afisa elimu Bi. Froliana Ntikahavuye, Bw. Elisha bagwanya, Masoud Kitowe na Abdallah Ntahuga.
Mkutano mkuu wa sita wa chama cha mapinduzi wilaya ya Kasulu ulifanyika katika ukumbi wa chuo cha ualimu Kasulu na kuendeshwa kwa amani na usalama ingawa kulikuwa na malalamiko kidogo ya wajumbe kutopata usafiri wa uhakika kutoka vijijini.
Miongoni mwa waliohudhuria mkutano huo ni pamoja na wabunge wote wa wilaya ya Kasulu Bw. Daniel Nsanzugwanko ambaye ni naibu waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Bw. Kilontsi Mporogomyi wa jimbo la Kasulu Magharibi na Mbunge wa viti maalumu Bi. Josephine Ngenzabuke.
Aidha gari moja lililokuwa limebeba wajumbe kutoka kata ya Rungwe mpya, liliacha njia na kuanguka na kusababisha majeruhi kadhaa waliopelekwa hospitali ya wilaya na kupatiwa matibabu na kisha kuruhusiwa, hakuna mtu aliyeripotiwa kufariki dunia.
Wengi wa watazamaji wa uchaguzi huo wameonesha kufurahishwa na mchakato huo wa uchaguzi na kukiri kuwa kulikuwa na ukomavu wa kisiasa ingawa vitendo vinavyoashiria kuwepo kwa rushwa vilitajwa kuwepo.
Wengi wa wanaCCM walitaja kuwa wajumbe wenye haki ya kupiga kura walikuwa wakiwashinikiza wagombea kuwapa fedha, chakula au vinywaji kama sehemu ya ushawishi wa kuwachagua katika nafasi walizoomba.