MSAFARA wa Waziri Kiongozi wa Zanzibar, Shamsi Vuai Nahodha, umemgonga mwanafunzi mmoja wa shule ya Sekondari ya Mission na kusababisha kuvunjika mkono.
Mwanafunzi aliyepatwa na mkasa huo ni farida Mhagama, ambaye anasoma kidato cha pili katika shule hiyo.
Hali hiyo ilitokea eneo la Mfaranyaki karibu na kituo cha mafuta cha Kisumapei, wakati msafara wa Vuai ukitokea Mbinga kuelelekea Manispaa ya Songea.
Ajali hiyo ilihusisha gari la polisi la Kituo cha Namtumbo, lenye namba PT 0833.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa, Benedict Ngaiza, alithibitisha hospitali hiyo kumpokea mwanafunzi huyo ambaye wamemfunga POP na kumpatia dawa za kupunguza maumivu.
Kaimu mkuu wa mkoa ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo, Gabriel Kimolo, aliyekuwepo katika msafara huo alifika hospitalini hapo kumpa pole mwanafunzi huyo na kuahidi kumgharamia matibabu.
Vuai yuko mkoani Ruvuma kwa ziara ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo na kwamba wakati ajali hiyo inatokea alikuwa akitokea kuzindua msikiti eneo la Litumbandesi.