SAKATA la makontena 74 miongoni mwa 261 yaliyokuwa na mchanga wenye madini yaliyozuiliwa na polisi kwa uchunguzi zaidi baada ya kubainika kuwa na utata, linaonekana kumwelemea Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI) Robert Manumba.
Manumba amekuwa akisita kuzungumzia suala hilo ambalo limekwishatolewa maelezo yanayopingana na viongozi kadhaa wa serikali, kwa takribani wiki moja sasa na hata anapopatikana kupitia simu yake ya kiganjani, amekuwa akikwepa kutoa kauli yoyote kuhusu utata huo.
Awali ilielezwa na Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Protas Mmanda kuwa makontena hayo yaliyokuwa yasafirishwe nje ya nchi, Mei mwaka huu na Kampuni ya Barrick Gold, yalifanyiwa ukaguzi na Idara ya Forodha na Ushuru ikishirikiana na Jeshi la Polisi.
Kwamba ukaguzi ulifanyika baada ya kupokea taarifa kutoka kwa wakala wa usafirishaji wa kampuni hiyo kuwa, kulikuwa na wasiwasi kuwa makontena hayo yalifunguliwa wakati yakisafirishwa kwenda katika bandari ya Dar es Salaam.
Mmanda katika taarifa yake kwa gazeti hili hakueleza ni matatizo gani yaliyokuwa katika kontena hizo, zaidi ya kueleza kuwa suala hilo lipo chini ya uchunguzi wa polisi.
Hata hivyo, katika hatua ya kustaajabisha, Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Kamishna Alfred Tibaigana, alikanusha taarifa ya Mmanda kwa kueleza kuwa Jeshi la Polisi, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam halikuhusika na uchunguzi wa kontena hizo na kutaka suala hilo aulizwe DCI Manumba.
Jitihada za gazeti hili kumpata Manumba kwa wiki nzima sasa ili aweze kuzungumzia suala hilo zilishindikana, ambapo kila mara lilipofika ofisini kwake, wasaidizi wake walieleza kuwa ana kazi nyingi, yuko nje ya ofisi ama yuko kwenye kikao.
Alhamisi wiki hii, gazeti hili lilifanikiwa kuzungumza naye kwa simu yake ya kiganjani na kumtaka mwandishi afike ofisini kwake Ijumaa asubuhi ili atoe tamko kuhusu suala hilo, hata hivyo mwandishi alisubiri kwa saa nne bila kuonana na Manumba.
Jana, Manumba alipopigiwa simu, alipokea na alipoulizwa kama yuko tayari kuzungumzia suala hilo, alisema hayuko katika nafasi ya kuzungumza kwa vile yuko msibani na kutoa ahadi nyingine tena ya kukutana na mwandishi ofisini kwake kesho Jumatatu.
Kwa mujibu wa taarifa za TRA, mpaka sasa makontena 190 kati ya 261yalionekana kuwa hayakuwa na matatizo, hivyo kuruhusiwa na mamlaka husika kuendelea na safari ya kusafirishwa nje.
Lakini taarifa nyingine zilizolifikia Tanzania Daima Jumapili zilieleza kuwa, makontena hayo yalikuwa yakisafirishwa kinyemela, bila kufanywa ukaguzi wa aina yoyote na mamlaka zinazohusika.
Taarifa za TRA zilikanusha tuhuma hizo na kusema kuwa makontena hayo hayakuruhusiwa kinyemela kama inavyodaiwa, bali taratibu zote za kiforodha zilizingatiwa, kama inavyofanywa kwa mchanga wa namna hiyo.