WAJUMBE wa Kamati Kuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), wamefanyiwa semina ya siku moja kuhusu mpango wa ‘CHADEMA ni msingi - tumaini jipya la Watanzania’.
Semina hiyo iliyofanyika jana katika Ukumbi wa Haidery Plaza, Dar es Salaam, itafuatiwa na kikao cha siku mbili cha kamati kuu cha chama hicho, kilichopangwa kuanza leo.
Akizungumza na Tanzania Daima jana, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa, alisema lengo la semina hiyo ni kuwaelimisha wajumbe hao, ili baadaye waweze kuutekeleza mpango huo kwa vitendo.
Alisema lengo la mpango huo ni kuwa na viongozi kuanzia ngazi ya msingi (balozi wa nyumba kumi kumi), kwa lengo la kuimarisha chama.
“Hatua hii inatokana na mabadiliko ya katiba ya chama yaliyofanyika mwaka jana, lengo ni kuwa na viongozi kuanzia ngazi ya msingi,” alisema Dk. Slaa.
Dk. Slaa alisema baada ya semina hiyo, itafuatiwa na kikao cha siku mbili cha kamati kuu ambacho kitapokea taarifa mbalimbali za sekretarieti, kutathmini hali ya siasa nchini na kuweka mikakati mbalimbali ya kuimarisha chama.