KITENDO cha Rais Jakaya Kikwete kupima hadharani virusi vinavyosababisha maradhi ya ukimwi, kimemkosha mke wa Rais wa Marekani, Laura Bush, ambaye amemwandikia rais barua ya kumpongeza.
Nakala ya barua hiyo ya Julai 27 mwaka huu, ilitawanywa jana kwa vyombo vya habari na Ikulu.
Katika barua hiyo, Laura Bush amemmwagia sifa Rais Kikwete na kusema kuwa, kitendo chake cha kujitokeza hadharani na kupima, kinafaa kuigwa na viongozi wengine Afrika na duniani kwa jumla.
“Kujitoa kwako kwa ajili ya kuzuia maambukizi ya HIV kumeonyeshwa kupitia uamuzi wako na mkeo, Mama Salma Kikwete, kuwa watu wa kwanza kupimwa siku ya kuzindua mpango huo,” anasema Laura Bush katika barua hiyo ya kurasa moja.
Aidha, mke huyo wa Rais wa Marekani, anasema kuwa Watanzania wanatakiwa kutekeleza kwa vitendo kauli iliyotolewa na Rais Kikwete siku ya uzinduzi wa mpango wa kupima virusi vya ukimwi, ya kuwataka kuacha unyanyapaa dhidi ya watu wenye virusi vinavyosababisha ukimwi.
Laura aliwataka Watanzania kumwamini Rais Kikwete aliposema kuwa matibabu kwa watu watakaobainika kuambukizwa virusi hivyo yapo na kwamba matibabu hayo yatawapatia maisha mazuri.
Alisema kuwa, kupitia Mpango wa Rais Bush wa kupambana na ukimwi (PEPFA), Marekani ipo tayari kuwa mshirika wa Tanzania katika kupambana na maradhi hayo.
“Kama ninyi, Marekani inaamini katika kupanua huduma za kupima kwa hiari na ushauri nasaha,” anasema Laura na kuongeza kuwa, mwaka jana, Serikali ya Marekani ilifadhili vituo vya upimaji 200 na hivyo kufanikisha kuwafikia watu 400,000 nchini.
Alisema kuwa mwaka huu, Marekani itaisaidia Tanzania katika jitihada zake za kupima watu 700,000.
“Tupo pamoja nanyi katika kuzuia maambukizi mapya, kuwatibu wale wanaoishi na HIV/ukimwi na kuwahudumia walioambukizwa HIV/ukimwi,” alisema.
Aidha, Laura alimuhakikishia Rais Kikwete kupitia barua hiyo kuwa, Marekani ipo tayari kusaidiana na Tanzania katika maeneo hayo katika utekelezaji wa dhamira yake ya kuona kuwa siku moja, Tanzania isiyo na ukimwi inawezekana.
Mpango wa kitaifa wa upimaji wa hiari wa virusi vya ukimwi, ulizinduliwa mapema mwezi huu na Rais Kikwete kama sehemu ya mpango wa Umoja wa Mataifa unaoyataka mataifa kubuni mipango kama hiyo ya kitaifa mwaka huu.