POLISI wilayani Tarime Mkoa wa Mara, wamefanikiwa kuzima mapigano ya koo za Wanchari na Wakira, baada ya kuwakutanisha viongozi na wananchi wa pande zote katika eneo la mapigano la Nyabichune.
Akizungumza na waandishi wa habari katika maeneo ya vijiji vya Remagwe na Ng’ereng’ere, hivi karibuni, Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Stanley Kolimba, alisema alfajiri ya Julai 24, kundi la watu wenye silaha za jadi kutoka Kijiji cha Korotambe, Kata ya Mwema, walivamia vijiji vya Ng’ereng’ere na Remagwe kwa nia ya kuvuna mahindi ya koo za Wakira na kuiba ng’ombe.
Alisema, wananchi wa vijiji vilivyovamiwa walipiga kelele za kuomba msaada na wengine kupiga simu Kituo cha Polisi Sirari na baada ya muda mfupi, polisi wakiwa wamejiandaa kuzima mapigano walifika eneo la tukio.
“Wanchari zaidi ya 300 walifika kwenye vijiji vya Wakira alfajiri sana wakiwa na silaha za kivita kwa lengo la kuvuna mahindi na kuiba mifugo ya Wakira… walipoona hivyo walipiga yowe na wengine kupiga simu polisi,” alisema Kolimba.
Alisema, waliwakutanisha viongozi wa vijiji vitatu na wananchi wa pande zote mbili waliokuwa na silaha tayari kwa mapigano na kuanza kutoa elimu ya hasara za mapigano kwao na serikali pia, hivyo waliwashauri kuweka silaha chini na kurudi makwao.
Aidha, polisi wilayani hapa wanaendelea na doria katika maeneo ya vijiji hivyo kwa kuwatawanya wananchi hao ili kuhakikisha hali inaendelea kuwa tulivu.
Wakati huo huo, Jeshi la Polisi limethibitisha kuokotwa kwa maiti ya Sande Matutu (41), mkazi wa Sirari aliyekuwa mtuhumiwa kwa vitendo vya ujambazi katika mipaka ya Tanzania na Kenya.
Ilielezwa kwamba, mwili huo ulikutwa na majeraha ya mshale wenye sumu kifuani na umehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Tarime. Uchunguzi wa polisi kuhusu tukio hilo unaendelea.