UPANUZI wa umeme wa gridi ya taifa kutoka kituo cha Makambako hadi Songea na kisha kupeleka umeme huo Wilaya ya Mbinga, Namtumbo na Ludewa utagharimu dola milioni 50.
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, William Ngeleja, aliliambia Bunge jana kuwa, upembuzi yakinifu kwa ajili ya mradi huo wa umeme ulikamalika mwanzoni mwa mwaka huu.
Alisema serikali inakamilisha majadiliano na serikali ya Sweden ya kupata fedha za ujenzi wa mradi huo.
Ngeleja alikuwa akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Pindi Chana (CCM), aliyetaka kujua mradi huo wa umeme utagharimu kiasi gani.
Katika swali lake la msingi, mbunge huyo alitaka kufahamu serikali ina mpango gani wa kupeleka umeme wilayani Ludewa, ili kuwawezesha wawekezaji waone madini ya chuma cha Liganga, dhahabu na makaa ya mawe ya Mchuchuma.
Akijibu swali hilo, Ngeleja alisema serikali kupitia Tanesco inatekeleza mradi wa kuyapatia umeme Makao Makuu ya Wilaya ya Ludewa.
Alisema kazi ya ujenzi wa miundombinu ya umeme ilianza Februari 2006 na ilipangwa kutekelezwa katika awamu mbili. Awamu ya kwanza ilihusisha upimaji wa njia ya kupitisha miundombinu, ujenzi wa sehemu ya miundombinu ya umeme na ukarabati wa jenereta ya halmashauri ya wilaya ambayo awali ndiyo ilikuwa itakayotumika kuzalishia umeme.
Alisema awamu ya pili itahusisha ununuzi na ufungaji wa jenereta mbili zenye uwezo wa KvA 1,250 kila moja ambazo zitawasili katika kipindi cha wiki 55 kuanzia Agosti mwaka huu.