SPIKA wa Bunge, Samuel Sitta, jana alitangaza kuwa siku ya Jumamosi itakuwa ni maalumu kwa wabunge wote kupima afya zao kujua kama wameambukizwa virusi vinavyosababisha ukimwi au la.
Akizungumza mara baada ya kipindi cha maswali na majibu bungeni jana, Sitta alisema kuwa, upimaji huo ni sehemu ya mwitikio wa kampeni ya kitaifa inayomtaka kila Mtanzania kupima ili kujua hali yake kiafya.
Akitoa tangazo hilo, Sitta alisema kuwa yeye mwenyewe atakuwa wa kwanza kupima, hivyo hakuna mbunge yeyote atakayekuwa na sababu ya kutofika siku hiyo na kupima afya yake.
Alisema zoezi hilo la upimaji litaanza majira ya saa 3:00 asubuhi baada ya kumalizika kwa mbio za wabunge za kilomita tano zitakazoanzia kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini hapa na kuishia katika viwanja vya Bunge.
“Ili nihakikishe wabunge wote mnapima mimi nitaongoza zoezi hilo la kupima kwa kuwa mpimaji wa kwanza,” alisema Spika.
Alibainisha kuwa zoezi la upimaji linapaswa kuwa la wazi na litafanyika mbele ya watu kama alivyofanya Rais Kikwete wakati wa uzinduzi wa kampeni hizo, Jumamosi iliyopita.
Alisema uwazi huo utasaidia pia wananchi kuona mfano utakaoonyeshwa na wawakilishi wao.
Wakati huo huo wakazi wa mji wa Dodoma wameonyesha kuhamasika kupima afya zao baada ya kuona Rais Kikwete akijitokeza kupima hadharani.
“Tumehamasika sana na naamini wananchi wengi watajitokeza kupima, maana kitendo cha Rais kupima hadharani kinatia moyo,” alisema.
Walisema awali walikuwa wakiogopa kupima kwa kujua kwamba mtu akikutwa na virusi vya ukimwi atakufa mapema kutokana na unyanyapaa uliokuwepo katika jamii.
Walisema hivi sasa jamii imeelimishwa kwa kiasi kikubwa kuhusu kuondoa unyanyapaa kwa waathirika na umuhimu wa kupima ili kujua afya zao.
Walisema utoaji wa dawa za ARV’s pia umeongeza kasi ya kupima kwani wananchi wameelewa kwamba, wakikutwa na maambukizi hautakuwa mwisho wao wa kuishi kutokana na kuwepo kwa dawa za kurefusha maisha kwa waathirika wa ukimwi.
Waliitaka serikali kutoa adhabu kali kwa watumishi wa sekta ya afya ambao hawawezi kutunza siri za wagonjwa na watu wanaokwenda kupima kwani wao ni kichocheo cha kuwafanya wananchi waogope kujitokeza kwenda kupima afya zao.
Wakazi hao wa mjini Dodoma walisema ni vema zoezi hilo la upimaji wa afya liendeshwe pia katika maeneo ya vijijini kwani wagonjwa hawapo mijini pekee, maana kutowapima wananchi wa vijijini ni kurudisha nyuma vita dhidi ya ukimwi.