SIKU chache baada ya Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe (Chadema) kuibua kashfa dhidi ya Waziri wa Nishati na Madini, Nazir Karamagi, kusaini mkataba wa madini nje ya nchi, baadhi ya wananchi wamependekeza kiundwe chombo ambacho kitawashinikiza viongozi wenye kashfa kulazimishwa kujiuzulu.
Kabwe alisema bungeni na baadaye waziri huyo kukiri kuwa alisaini mkataba wa madini kati ya serikali na Kampuni ya Barrick Gold Mine kwa ajili ya mgodi wa Buzwagi jijini London, badala ya Dar es Salaam.
Akizungumza na Tanzania Daima jana, Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi wa Shughuli za Meli na Bandari Tanzania (DOWUTA), Abdallah Kibunda, alisema ikiwa chombo hicho kikiundwa kitasaidia kwa kiasi kikubwa kurekebisha mambo mengi pia kutawezesha kuimarisha uchumi wa nchi.
“Jamii inapaswa kufanya jambo la kulinda heshima ya taifa hili mbele ya uso wa taifa lenyewe na kimataifa kwa kuunda chombo cha kushinikiza viongozi wa aina hiyo kuondolewa au kujiondoa wenyewe madarakani,” alisema Kibunda.
Sambamba na hilo, Kibunda alishauri pia wananchi kujizatiti kwa kuungana pamoja na wabunge wanaohoji vitendo vya baadhi ya viongozi kama mawaziri wanaotuhumiwa kuhujumu maendeleo ya nchi kama alivyofanya Waziri Karamagi.
“Sheria nyingi za kudhibiti maadili ya wakulima na wafanyakazi, kuna sheria za jinai na za kazi ambazo huwabana wafanyakazi ili waweze kuzizingatia na kufanya kazi kwa uadilifu kwa maendeleo ya taifa… mfanyakazi asiyezingatia hufukuzwa, kwa nini viongozi hawa wa kitaifa wasiachishwe kazi?” alihoji Kibunda.
Aliongeza kuwa viongozi wa hapa nchini wanajiona wapo juu ya sheria na wana uwezo mkubwa wa kufanya lolote lile wanaloliona lina manufaa kwao binafsi bila kujali athari ya matokeo ya vitendo vyao.
‘‘Hivi tujiulize, tunakwenda wapi? Kwa nini nchi hii tuitelekeze mikononi mwa viongozi wafanye watakavyo, viongozi ambao hawana utamaduni wa kuona haya wala kuwajibika mbele ya wapiga kura wao, kwa kweli tuhuma hizi dhidi ya serikali ni nzito na namna ilivyoisha bungeni inasikitisha, jamii inafanya nini katika jambo kama hili, inakaa kimya tu na kuona bora liende?” alihoji zaidi.
Naye Jerome Tilya, alisema jambo hilo lililofanywa na Waziri Karamagi linaonyesha ni namna gani viongozi wanavyojifanyia maamuzi nyeti kienyeji.
Alihoji majibu yaliyotolewa bungeni na waziri huyo kuwa amefanya hivyo kwa mazoea kwa kusema hali hiyo imeonyesha ni kwa kiasi gani viongozi wanavyokumbatia madaraka.
Mkazi mwingine wa Dar es Salaam, Salma Saidi, alimshauri waziri mkuu kuingilia masuala yanayopindishwa na viongozi wake kwani kwa kufanya hivyo kutasaidia kuweka mambo mengi sawa pia kuwafanya wananchi kuwa na imani na viongozi.
“Viongozi wetu wengi wamekuwa wakifanya mambo mengi ovyo ovyo na pale wanapohojiwa na kutakiwa wajiuzulu husimama vifua mbele na kupingana na matakwa ya wananchi au hata watendaji wao, tumewashuhudia baadhi ya viongozi ambao mara wanapogundulika kuwa wamevurunda na kutakiwa kujiuzulu hukataa, hivi wanapata wapi meno?” alihoji Salma.
Halfan Waziri alisema kuna haja kwa rais kukaa na watendaji wake na kuwaonya kuhusu masuala mbalimbali wanayoyapindisha hatimaye.