RAIS Jakaya Kikwete, amemteua Jaji wa Mahakama ya Rufaa Tanzania, Augustino Steven Lawrence Ramadhani, kuwa Jaji Mkuu mpya wa Tanzania.
Uamuzi huo wa rais, ulitangazwa jana kwa taarifa rasmi ya Ikulu iliyotiwa saini na Katibu Mkuu Kiongozi, Philemon Luhanjo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya Ikulu, kazi ya kumuapisha Jaji Mkuu huyo mpya, anayechukua nafasi ya Barnabas Samatta anayestaafu keshokutwa, inatarajiwa kufanyika kesho saa 10:00 jioni, Ikulu jijini Dar es Salaam.
Jaji Ramadhani mbali ya kuwa Jaji wa Mahakama ya Rufaa, alikuwa pia Makamu Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar.
Aidha, mwaka 2001 Jaji Ramadhani aliteuliwa kuwa miongoni mwa majaji sita wa Mahakama ya Rufaa ya Afrika Mashariki.
Takriban mwezi mmoja uliopita, nafasi ya Jaji Mkuu wa Tanzania ilikuwa ikikaimiwa na Jaji John Mrosso ambaye aliteuliwa kushika wadhifa huo kwa muda na Rais Jakaya Kikwete wakati Samatta akiwa nje ya nchi.
Wakati huo huo, Msajili wa Mahakama ya Rufani, Sophia Wambura, alisema Mahakama ya Tanzania kesho asubuhi itafanya kikao maalum cha kumuaga Jaji Samatta kitaaluma kwenye Jengo la Mahakama ya Rufani lililopo Kivukoni Front, jijini Dar es Salaam.
Baada ya kikao hicho, Jaji Mkuu Samatta atakagua gwaride la heshima mbele ya jengo la mahakama na viongozi mbalimbali wa serikali na majaji wanatarajiwa kuudhuria.
Samatta aliteuliwa kuwa Jaji Mkuu mwaka 1999, akichukua wadhifa huo kutoka kwa Francis Nyalali aliyekuwa Jaji Mkuu wa kwanza Mwafrika hapa nchini.