MCHUNGAJI Peter Gabriel na wenzake watatu waliotuhumiwa kufukua maiti ya Samweli Limbu wilayani Kahama wamehukumiwa kwenda jela miaka minne.
Akitoa hukumu hiyo, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Wilaya ya Kahama, Ismael Ngalie, alisema watuhumiwa hao wanne, Limbu Manoti, Anastazia Limbu, Peter Gabrieli pamoja na Paulo Joseph walikuwa wakikabiliwa na mashitaka mawili kila mmoja.
Alisema Aprili 21 mwaka huu katika Kijiji cha Nyasubi wilayani Kahama, majira ya saa 2:00 usiku washitakiwa walikwenda katika makaburi ili kufukua maiti huku wakidai kuwa, wameshukiwa na nguvu za Yesu.
Hakimu Ngalie alisema mashitaka waliyokuwa wakikabiliwa nayo ni kupanga njama za kufukua maiti ya Samweli Limbu na kosa la pili likiwa ni kuizuia maiti ya marehemu isiweze kuzikwa tena.
Hukumu ya hakimu huyo ilikuja baada ya Mwendesha Mashitaka, Mkaguzi wa Polisi Elias Haway, kuiomba mahakama itoe adhabu kali kwa watuhmiwa hao, kwani kitendo walichokifanya ni cha kinyume na Sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hivyo ingeweza kusababisha uvunjwaji wa amani katika sehemu hiyo.
Aliendelea kuiambia mahakama kuwa, kitendo hicho pia kingeweza kusababisha matabaka makubwa katika dini, pamoja na kuhatarisha maisha ya polisi waliokwenda kuhakikisha amani inakuwapo katika tukio hilo ambalo lilivuta hisia za wakazi wa mji wa Kahama.
Kumekuwa na mfululizo wa matukio kama hayo ya ufukuaji wa maiti katika Wilaya ya Kahama, kwani hivi karibuni, mganga mmoja wa asili kutoka katika Kijiji cha Busangi alifikishwa mahakamani kwa kosa la kutaka kufukua maiti kwa ajili ya kuifanyia shughuli za kiganga.