BAADHI ya maeneo ya Mkoa wa Arusha kwa siku mbili mfululizo, yamekumbwa na tetemeko la ardhi ambalo halijawahi kutokea katika maeneo hayo kwa miaka mingi.
Baadhi ya watu waliozungumza na mwandishi wa habari hizi, walisema maeneo yaliyotikiswa na tetemeko hilo lililotokea nyakati za usiku kati ya saa 5:00 na saa 9:00, ni pamoja na Mto wa Mbu na Engaruka.
Taarifa nyingine zinasema tetemeko hilo liliyakumba pia maeneo ya Longido ambako kama ilivyo katika maeneo mengine hakukuwa na madhara yoyote yaliyotokea.
Huko Engaruka, moja ya maeneo ambayo yametajwa kukumbwa na dhoruba hiyo ambayo inaweza ikahusishwa na harakati za kivolcano katika eneo hilo lililo jirani na Mlima Kilimanjaro, Eldonyo Lengai na maeneo ya Ngorongoro ni Kijiji cha Selela. Hali hiyo ilisababisha Mkuu wa Wilaya ya Mondolu, Luteni mstaafu, Issa Machibya alazimike kutembelea maeneo yaliyokumbwa na tetemeko hilo ili kubaini kiwango cha athari.
Akizungumzia hali hiyo, Machibya alisema na kubaini kutokuwapo kwa athari zozote kubwa za wazi zilizotokana na tetemeko hilo na kwamba iwapo lolote litabainika taarifa zaidi zitatolewa.
Habari nyingine zinaeleza kuwa, tetemeko jingine la ardhi lilisikika kutikisa maeneo mengine kadhaa ya Mkoa wa Dodoma jana alfajiri, ingawa kulikuwa hakuna taarifa za wazi kuhusu hali hiyo.