WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Ikulu, Dk. Mwinyihaji Makame, amesema amesikitishwa na kitendo cha Waziri wa Fedha wa Serikali ya Muungano, Zakia Meghji kutotekeleza ahadi yake ya kusaidia bajeti ya Zanzibar katika mwaka wa fedha 2006/07 kama alivyoahidi.
Aliyaeleza hayo juzi alipokuwa akijibu swali la Mwakilishi wa Jimbo la Koani, Mkema Haji Mkema (CCM), katika kikao cha Baraza la Wawakilishi kinachoendelea mjini hapa.
Dk. Mwinyihaji aliwaeleza wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, kwamba Waziri Meghji katika bajeti yake ya mwaka 2006/07 aliahidi kusaidia bajeti ya Zanzibar kutokana na uchumi wake kuwa mdogo, lakini hadi sasa hakuna kilichofanyika katika utekelezaji wa ahadi hiyo.
Waziri Makame alisema kwamba pia ahadi hiyo baadaye ilitiliwa mkazo na Rais Jakaya Kikwete kwa kuzingatia kwamba uchumi wa Zanzibar ni mdogo kulinganisha na ule wa Tanzania Bara, lakini hadi sasa Zanzibar haijapokea fedha hizo za kusaidia bajeti.
“Mheshimiwa Spika hata mimi sijafurahi, lakini sina la kuongeza hivi sasa kwa sababu bado fedha hazijatolewa,” alisema Waziri Makame.
Hata hivyo, aliwaeleza wajumbe wa Baraza hilo kuwa, katika mwaka wa fedha unaomalizika, Zanzibar ilipokea kama kawaida mgawo wake wa msaada wa asilimia 4.5 kutoka kwa wahisani kupitia misaada inayotolewa kupitia mfuko wa Serikali ya Muungano.
“Zanzibar imenufaika na kiasi cha sh bilioni 8 kutokana na msamaha wa madeni ya nje,” alisema Dk. Mwinyihaji.
Aliwaeleza wajumbe wa Baraza hilo kuwa serikali imepanga kuzitumia fedha hizo za msamaha katika kununua pembejeo za kilimo, vifaa vya maji na magari ya serikali.
Alisema hivi sasa serikali za Zanzibar na Muungano zinaendelea kuzungumzia juu ya fedha zinazotarajiwa kutolewa na Serikali ya Marekani kupitia mpango wa Millenium Challenge (MCA) juu utaratibu wa mgawo.
Waziri Meghji aliahidi kusaidia fedha bajeti ya Zanzibar ya mwaka 2006/07 alipokuwa akiwasilisha bajeti yake katika Bunge la Muungano kwa vile uchumi wa Zanzibar ni mdogo.