UONGOZI wa Hoteli ya White Sands Resort umetiwa mbaroni kwa tuhuma za kujipatia huduma ya maji kinyume cha taratibu na kuisababishia hasara Mamlaka ya Maji Safi na Maji Taka Mkoa wa Dar es Salaam (DAWASCO).
Hali hiyo ilitokea jana wakati polisi walipomchukua mhandisi wa hoteli hiyo, Raamy Shandra na kumpeleka katika kituo kidogo cha Polisi Kawe, baada ya kukiri kujiunganishia maji isivyo halali.
Shandra, alikiri kosa na kueleza sababu za kufanya hivyo kuwa ni nguvu ndogo ya maji katika eneo lao.
Aidha, Meneja wa DAWASCO kituo cha Kawe, Eneliko Mulokozi, aliithibitishia Tanzania Daima kuwa hoteli hiyo ni miongoni mwa wahujumu wa maji kwa muda mrefu kiasi cha kujifungia mota ili kuvutia maji mengi.
“Wametumia njia ya maji tuliyounganisha kwa kukata bomba na kuweka ya mota ya umeme yenye nguvu ya hp2 inayosambaza maji eneo la hoteli na eneo la jirani la Water n’ Wild,” alisema Mulokozi.
Ofisa Uhusiano wa DAWASCO, Badra Masoud, alisema ni lazima waifikishe hoteli hiyo kwenye vyombo vya sheria kwa kuwa wizi wa maji ni tatizo sugu katika Jiji la Dar es Salaam na maeneo jirani.