MKOA wa Singida, umeshika nafasi ya kwanza kwa umaskini uliokithiri hapa nchini katika kipindi cha mwaka mmoja.
Hayo yamesemwa na Katibu Tawala Msaidizi wa huduma za uongozi na usimamizi, Sebastian Mundia, alipokuwa akitoa taarifa kuhusu mikopo ya wajasiriamali wadogo kupitia mfuko wa uwezeshaji wa wananchi.
Alisema, katika kipindi hicho, wakazi wa mkoa huo walikopa jumla ya sh 341,373,150 kati ya sh bilioni moja za mfuko wa uwezeshaji wananchi kiuchumi na kukuza ajira zilizotolewa na Rais Jakaya Kikwete.
Mundia, alieleza kuwa hadi sasa wananchi wa Singida vijijini walikopa sh milioni 1.5; Manispaa ya Singida sh milioni 78.1; Manyoni sh 161,609,150 wakati Iramba ilikopa sh 100,164,000.
Hata hivyo, jumla ya vikundi vya kiuchumi, watu binafsi na vyama vya akiba na mikopo (SACCOS) 3,287 vimewasilisha maombi ya mikopo yenye thamani ya sh 12,176,092,182 katika benki za NMB na CRDB.
Alitaja baadhi ya mikakati ya kufanikisha zoezi hilo kuwa ni kutoa mafunzo kwa wawezeshaji wa wilaya, kamati za maendeleo ya kata, wataalamu wa maendeleo vijijini na kuhamasisha wananchi kuweka mazingira ya kukopesheka kwa kuanzisha vikundi vya vyama vya ushirika vya kuweka na kukopa (SACCOS).
Aidha, alitoa taarifa hiyo juzi kwenye semina ya siku moja iliyoitishwa na Wizara ya kazi, ajira na maendeleo ya vijana iliyohusu mwongozo kuhusu utaratibu wa wajasiriamali kuomba mikopo kutoka mfuko wa uwezeshaji.
Hivi karibuni Waziri Mkuu Edward Lowassa, alisikitishwa na kasi ndogo ya utoaji mikopo kutoka katika fedha za Rais Kikwete, alizozitoa kwa kila mkoa.