MKUU wa Jeshi la Polisi Tanzania, Inspekta Jenerali Said Mwema, ametangaza mkakati wa maeneo manne yatakayosaidia kudhibiti ujambazi na uhalifu nchini.
IGP Mwema alitangaza maeneo hayo kuwa ni kuzuia na kudhibiti uhalifu, kujenga mahusiano na wananchi, vifaa na mawasiliano ya polisi, na mwisho mazingira ya kufanyia kazi kwa polisi.
Alikuwa akifanya mkutano na wahariri na wakurugenzi wa vyombo vya habari nchini kwenye ukumbi wa hoteli ya Millennium Tower, Dar es Salaam, jana.
Alifafanua kuwa, jeshi hilo linahitaji teknolojia ya kisasa itakayosaidia kubaini na hatimaye kudhibiti uhalifu, suala alilosema ni muhimu kweli: “Hili ukiniuliza leo unisaidie nini, ndilo nitataja likiwa la kwanza… vyombo na nyenzo za kisasa,” alisema.
Alisisitiza kuwa inatakiwa polisi wajenge uhusiano bora na wananchi, watunze siri za watuhumiwa, hata hivyo akawasihi wananchi nao wasiwe chanzo cha kutoa siri zao kwa nia ya kutamba.
“Unakuta mtu anapeleka taarifa polisi, akirudi anaanza kutamba mtaani. Anasema subirini mtaona, kuna kitu kitatokea hapa… kwenye teksi aliyopanda anaeleza bila kujua anazungumza na nani, anamweleza yote anayofanya na polisi, hii itavujisha habari zako,” alisema.
Kuhusu mazingira ya polisi kufanyia kazi, alisema mazingira yanaweza kuwachanganya askari wake, kwani mtu analala katika nyumba isiyo salama, hana usafiri na hilo linaweza kuwa chanzo cha utendaji wao kushuka.
Hata hivyo, alisema serikali ya sasa imejizatiti kuhakikisha inawawezesha polisi walau waishi maisha yatakayowafanya waheshimike katika jamii na tayari juhudi zimeanza kuonekana.
Pia, baada ya kuelezwa kuwa katika Jeshi la Polisi mwandishi wa jeshi hilo, Mohamed Muhina, ndiye pekee anayeonekana kufanya kazi na wengine hawasikiki, Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, Paul Chagonja, alisema atahakikisha majina na namba zao zinatangazwa hadharani, suala lililopingwa na IGP.
“Kwa nini uende kutafuta watu. Chamsingi hapa ni kufanya utaratibu akawezeshwa kuongoza kitengo hicho. Kamishna umesikia, fanya utaratibu Muhina aongezewe nguvu. Hatuwezi kwenda kutafuta watu wanaojificha, mpe nguvu anayeonekana wazi,” alisema Mwema.
Agizo hilo lilimaanisha kuwa IGP ametaka Muhina aongezewe cheo kutoka cheo chake cha sasa cha Staff Sergeant kwenda juu zaidi. Mwema alisisitiza mwishoni mwa kikao na wahariri kuwa mengi yaliyojadiliwa pale yaliyo katika uwezo wa polisi yatekelezwe mara moja likiwamo hilo la Muhina, na majibu yapatikane haraka.
Kwa upande wa wahariri, walishauri masuala mbalimbali ikiwamo ombi rasmi waliloliwasilisha kwa Mwema kuwa, polisi wakopeshwe pikipiki ziwasaidie katika usafiri wa kazi na binafsi, suala alilokubaliana nao.
Pia, waliomba polisi wa chini wapewe mafunzo maalum, waache kupambana na waandishi wa habari, wajenge ushirikiano, suala aliloliunga mkono na kupendekeza iundwe kamati ya pamoja kati ya polisi na vyombo vya habari.
Pia, waliomba Jeshi la Polisi nchini kuangalia uwezekano wa kusajili namba za simu za mkononi za watumiaji wote kuepusha matumizi mabaya, ikiwamo kutumika katika ujambazi, suala alililolipokea pia.
Wahariri walilipongeza jeshi hilo kuwa limeanza kubadilika na sasa linatia matumaini kuwa litafanya kazi vyema baada ya kuondoa mapungufu hayo madogo.