Na Epson Luhwago
MBUNGE wa Same Mashariki (CCM), Anne Killango Malecela amewataka Wabunge na watu wanaombeza Waziri wa Maji Stephen Wassira kuwa ni mzee waache mara moja.
Anne alisema hayo juzi alipokuwa akichangia hotuba ya makadirio ya matumizi ya ofisi ya Waziri Mkuu na asasi zilizo chini yake , akiwa mtu wa pili kuchangia baada ya mume wake, John Malecela (Mtera-CCM).
Alisema baadhi ya watu wamekuwa wakimbeza Waziri huyo kuwa ni mzee na kwamba hawezi kuhimili kasi ya serikali ya awamu ya tatu kutokana na umri wake.
"Wanaosema Wassira mzee waache kabisa mara moja. Kuwa kijana siyo kufanya kazi. Kwanza napenda MheshimiwaNaibu Spika kukufahamisha kuwa hakuna mchapakazi kamaWassira. Ukimpelekea suala asubuhi jioni unapewa jibu,"alifafanua.
Katika mchango wake, Anne aliwasihi Wabunge wenzake kuhudhuria vikao vya Halmashauri za Wilaya, Miji na majiji katika majimbo yao ili kuwabana ipasavyo watendaji wabovu katika halmashauri hizo.
Alisema baadhi ya watendaji katika halmashauri wamekuwa jeuri kutokana na kutokuwepo watu wa kuwabana hususan Wabunge. Alisema kama Wabunge watawabana watendaji hao kazi za serikali katika maeneo hayo zitafanyika ipasavyo.
Kuhusu maendeleo katika wilaya zenye majimbo mawili au zaidi, Anne alisema serikali haina budi kuweka uwiano mzuri mgawanyo wa raslimali na mipango ya maendeleo katika majimbo yote bila kujali yanaongozwa na watu gani.
"Utakuta katika baadhi ya wilaya kuna majimbo mawili au zaidi. Lakini moja linaendelea au linawekewa vipaumbele vingi kuliko mengine. Hali hii itatufanya tujenge paradiso na jehanamu ndani ya wilaya moja kwa kuwa sehemu zingine zitakuwa zimeendelea na zingine maskini," alisema.
Kwa upande wa miundombinu, alisema serikali haina budi kuwekeza zaidi katika ujenzi wa barabara hususan za vijijini kwa kuwa ni msingi wa maendeleo katika maeneo mbalimbali.
Alisema katika jimbo lake, mathalan kuna barabara mbovu hali inayowafanya wananchi wake kuendelea kuwa katika umaskini wa kutupwa licha ya kuwa ni wazalishaji wazuri wa mpunga na mahindi.
Naye John Malecela, ambaye alifungua pazia la kuchangia hotuba hiyo inayotarajiwa kuchangiwa na Wabunge 90, alisema ni vyema serikali ikaweka mipango madhubuti ya upatikanaji wa huduma za maji safi kwa wananchi.
Alisema pamoja na kuwepo mipango kamambe ya kupatikana kwa huduma hiyo, wananchi katika maeneo mbalimbali ya nchi bado wanafuata huduma hiyo kwa takriban kilomita 10.
Kuhusu ongezeko la watoto wa mitaani ambao alisema miongoni mwao hutokana na wazazi kudai kuwa siyo wao, alishauri mashine za kupimia damu (DNA) zitafutwe kwa wingi ili pindi unapotokea mzozo baina ya wanandoa basi vipimo hivyo vitumike mara moja.