JESHI la Polisi nchini limefanikiwa kukamata madereva na leseni feki wakati wa ukaguzi wa leseni na kuhakiki uzima wa magari hayo ili kukabiliana na tatizo la ajali.
Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP), James Kombe, alithibitisha kukamatwa kwa magari hayo baada ya operesheni iliyofanywa kwa ushirikiano kati ya polisi na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA).
“Kwa ujumla operesheni hii imefanikiwa kwa kiasi na si kwa Mkoa wa Dar es Salaam peke yake kwani inafanyika katika mikoa yote hapa Bara,” alisema Kamishna Kombe.
Alisema, katika ukaguzi uliofanyika Dar es Salaam, polisi wamefanikiwa kuwakamata madereva feki 30 kati ya magari 968 wakati mjini Moshi, walipata leseni 10 za kughushi katika magari 162 yaliyokamatwa.
Katika hatua nyingine, Kamishna Kombe, ameuagiza uongozi wa jiji kupanga upya utaratibu wa uegeshaji mabasi makubwa yaendayo mikoani na nchi jirani ndani ya kituo kikuu cha mabasi, Ubungo.
“Tayari nimeshaiagiza mamlaka husika kushughulikia suala hili kwa haraka kwa kuwa kumekuwa na mkanganyiko wa mabasi hayo, jambo linalosababisha usumbufu kwa abiria.
“Nimeagiza, mabasi yanayokwenda Kanda ya Ziwa yawe na sehemu yake, ya Kusini yawe na mahali pake…na yale ya Kanda ya Kati, Kaskazini, Nyanda za Juu bila kusahau yale yanayokwenda nchi jirani, tunaamini itasaidia kuondoa usumbufu kwa abiria,” alisema Kamishna Kombe.
Alisema, kuwa lengo la utafiti huo ni kuhakikisha kuwa tatizo la ajali barabarani linapungua na hatimaye kwisha kabisa.
Katika siku za hivi karibuni watu 52 walipoteza maisha ndani ya kipindi cha wiki mbili kwenye ajali za barabarani.